Upimaji afya bure waibua msongamano

Muktasari:

  • Upimaji afya bure unafanyika katika meli iliyotia nanga katika Bandari ya Dar es Salaam.

 Upimaji afya bure unaofanywa na madaktari kutoka China katika Bandari ya Dar es Salaam umesababisha foleni kwa watumiaji wa barabara.

Upimaji wa afya unafanyika kwenye meli iliyotia nanga katika Bandari ya Dar es Salaam.

Katika Barabara ya Kilwa, magari yanayoelekea Posta na Gerezani yamekuwa yakitembea mwendo wa taratibu na kusimama kwa takriban kwa dakika 20 kabla ya kusogea.

Kondakta wa daladala linalofanya safari kati ya Mbagala Rangi Tatu na Stesheni, Yasin Yusuph amesema leo Jumatatu Novemba 20 kuwa wametumia zaidi ya saa mbili kwa safari.

"Sisi tumetoka Mbagala saa 1:30 hadi sasa saa 3:40 hatujafika na mwendo ni huuhuu unaouona wa taratibu. Magari yakishasimama unasahau. Tatizo ni kuwa hakuna utaratibu maalumu, watu wamejaa kila sehemu na wanaruhusu magari njia mbili," amesema Yusuph.

Amesema ni vyema lingetafutwa eneo kubwa ambalo watu wanaweza kukaa na kusubiri huduma badala ya kusimamishwa pembezoni mwa barabara.

"Watu ni wengi, eneo la kupumzika hakuna. Hapa hakuna miti ya kutosha jua likiwa kali litawachoma," amesema.