Utafiti: Idadi ya wanaoikubali Chadema yaporomoka kutoka asilimia 32 hadi 17

Muktasari:

  • Matokeo haya yametolewa na Twaweza leo Alhamisi, katika utafiti wake uitwao ‘Matarajio na matokeo; Vipaumbele, utendaji na siasa nchini Tanzania.’
  • Utafiti umebaini kuwa Chadema kinakubalika zaidi miongoni mwa vijana, wanaume, watu matajiri na wenye kiwango kikubwa cha elimu.

Dar es Salaam. Utafiti mpya uliofanywa na Taasisi ya Twaweza umebaini kuwa kukubalika kwa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kumeporomoka kutoka asilimia 32 mwaka 2013 hadi asilimia 17 mwaka huu.

Matokeo haya yametolewa na Twaweza leo Alhamisi, katika utafiti wake uitwao ‘Matarajio na matokeo; Vipaumbele, utendaji na siasa nchini Tanzania.’

Utafiti umebaini kuwa Chadema kinakubalika zaidi miongoni mwa vijana, wanaume, watu matajiri na wenye kiwango kikubwa cha elimu.

Kadhalika utafiti huo ulibaini kuwa CCM imeendelea kuimarika kwa kukubalika kwa kati ya asilimia 54 na 64 kati ya mwaka 2012 na 2017.

“Mwaka 2013 na 2014 kiwango cha kukubalika kilishuka na kilifikia asilimia 54 kutoka asilimia 65 ya 2012. Kukubalika kwa CCM kumeendelea kubaki katika kiwango hicho hicho cha asilimia 62 tangu uchaguzi wa mwaka 2015 na asilimia 63 mwaka 2017,” umesema utafiti huo.

Utafiti huo ulibaini, CCM inakubalika zaidi miongoni mwa wazee (asilimia 80), ukilinganisha na asilimia 55 ya vijana. Wanawake (asilimia 68) wanaikubali CCM kuliko wanaume (asilimia 58), maeneo ya vijijini (asilimia 66) kuliko maeneo ya mijini (asilimia 57), na wananchi masikini (asilimia 69) kuliko matajiri (asilimia 53).

Wananchi wenye elimu ya sekondari, elimu ya ufundi au elimu ya juu wanaikubali CCM kwa asilimia 46.