Utafiti kufanyika kubaini barafu kupungua Mlima Kilimanjaro

Muktasari:

  • Wanasayansi hawajajua kiini cha kupungua barafu katika Mlima Kilimanjaro na maeneo mengine yenye barafu nchini, hivyo utafiti utafanywa kwa kushirikiana na WMO na kuja na majibu.

Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) linatarajia kuanzisha kituo cha utafiti kubaini kiini cha kupungua barafu katika Mlima Kilimanjaro na maeneo mengine yenye barafu nchini.

Utafiti huo unalenga kupatikana taarifa na kuchukua hatua za kudhibiti hali hiyo isiendelee kutokea.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini (TMA), Dk Agnes Kijazi amesema hayo wakati wa mkutano wa  wataalamu na watafiti wa hali ya hewa kutoka WMO.

Amesema jana (Julai 4) kuwa hadi sasa wanasayansi hawajajua kiini cha kupungua barafu kwenye Mlima Kilimanjaro na maeneo mengine ya tropiki kwa sababu  hakuna kituo cha kukusanya takwimu za  utafiti.

Dk Kijazi amesema mkutano huo unajadili kupungua kwa barafu kwenye milima katika nchi za tropiki.

Amesema ili kukabiliana na ukosefu wa taarifa za takwimu za utafiti, WMO itaweka mashine za kupimia hali ya hewa na taarifa zake zitatumika kufahamu hali ya hewa duniani na mabadiliko ya tabia ya nchi.

Mkurugenzi huyo amesema kufungwa kwa mashine hizo kutawezesha kuanzishwa kwa kituo cha hali ya hewa Mlima Kilimanjaro na TMA imejipanga kwa mazungumzo na WMO yatakayowezesha kuanzishwa kituo cha utafiti huo wa kupungua kwa barafu.