Utafiti wabaini upungufu huduma afya ya uzazi

Muktasari:

Mwongozo wa wizara unaeleza kuwa mwanamke baada kujifungua anatakiwa kufanyiwa uchunguzi ndani ya saa 24

Dar es Salaam. Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Aga Khan, Eunice Pallangyo amefanya utafiti na kubaini kwamba vituo vya afya havitoi huduma ya uangalizi kwa kinamama baada ya kujifungua hali inayosababisha vifo vya uzazi kuongezeka.

Ripoti ya Jamii na afya (DHS) ya ofisi ya Taifa ya Takwimu kwa mwaka 2015/16 inaonyesha kuwa kuna vifo 556 vya uzazi katika kila vizazi hai 100,000 wakati kulikuwa na vifo 454;100,000 mwaka 2010/11.

Akizungumzia utafiti huo mbele ya wadau wa afya wa wilaya ya Ilala, Pallangyo amesema katika vituo vya afya 27 alivyotembelea hakuna huduma ya uangalizi wa kinamama baada ya kujifungua.

Amesema mwongozo wa Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto unaelekeza kuwa baada ya wajawazito kujifungua wanatakiwa kuwa katika uangalizi katika kipindi cha siku 42.

Kwa mujibu wa mwongozo huo, mwanamke baada kujifungua anatakiwa kufanyiwa uchunguzi ndani ya saa 24 baada ya kujifungua.

Alishauri Serikali kusimamia utekelezaji wa miongozo inayoweka kwa kuzungumza na watendaji ili kufahamu changamoto zinazowakabili.

Mkurugenzi wa Huduma za Uuguzi na Ukunga wa Wizara ya Afya, Gustan Moyo amesema Serikali imekuwa ikiboresha huduma za afya.

“Tumekuwa tuna upungufu wa watumishi wa afya, miundombinu na fedha, lakini Serikali imekuwa ikiboresha sekta ya elimu kwa kuiongezea bajeti yake, huduma zinaendelea kuimarika,” amesema.