Uteuzi wa Janeth Masaburi wapokewa kwa hisia tofauti

Muktasari:

  • Wasomi wasema ameona wabunge hawa watamvusha hadi 2020

Siku moja baada ya Rais John Magufuli kumteua Janeth Masaburi kuwa mbunge, wadau wametofautiana kuhusu uteuzi huo.

Uteuzi huo wa Rais Magufuli alioufanya juzi kwa mujibu wa Ibara ya 66 (1)(e) ya Katiba ya Tanzania inayompa mamlaka ya kuteua wabunge 10, umehitimisha nafasi hizo za uteuzi.

Profesa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Benson Bana alisema Rais Magufuli amejiridhisha kwamba timu aliyonayo inatosha kumfikisha mwaka 2020 na hakuona sababu ya kuacha wazi.

“Ukiangalia hata mabadiliko madogo ya baraza lake la mawaziri aliyoyafanya hivi karibuni hakuteua mtu kutoka nje,” alisema Profesa Bana.

Naye Mbunge wa Kawe, Halima Mdee alisema: “Unajua Rais kwa zile nafasi kumi anaweza kumteua yeyote lakini kwa hiki alichokifanya kwa Janeth ni sawa na kumpa hisani tu, kwani huyu aligombea ubunge wa viti maalumu mwaka 2015 na akatoswa.”

Akizungumzia uteuzi huo, Katibu mkuu wa TLP, Nancy Mrikaria alisema Rais Magufuli amemteua Janeth kwa kuzingatia Katiba inayompa uwezo huo. “Janeth anakwenda kuongeza idadi ya wanawake bungeni, niwaombe tu wabunge wanawake, waungane na kuwa kitu kimoja,” alisema Mrikaria.

Mwenyekiti wa chama cha ukombozi wa umma (Chaumma), Hashim Rungwe alisema: “Ni uteuzi wa ubaguzi na amemaliza nafasi zake za kuteua wa CCM, tumezoea huko nyuma wanateuliwa na wapinzani lakini sasa hakuna.”

Wabunge wengine walioteuliwa ni mawaziri ni; Dk Philip Mpango (Fedha na Mipango), Profesa Palamagamba Kabudi (Katiba na Sheria), Profesa Joyce Ndalichako (Elimu, Sayansi na Teknolojia), Profesa Makame Mbarawa (Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano), Dk Augustine Mahiga (Mambo ya Nje), Dk Tulia Ackson (Naibu Spika), Mama Salma Kikwete, Anne Kilango Malecela na Abdallah Bulembo.