VIDEO: ACT Wazalendo wapeleka barua kwa Spika kuhoji Sh1.5 trilioni

ACT WAZALENDO WAPELEKA BARUA KWA SPIKA KUHOJI SH1.5 TRILIONI

Muktasari:

Wamesema upinzani una wajibu wa kuhoji ili kuhakikisha  Watanzania wanajua fedha zao zinakwenda wapi.


Dar es Salaam. Chama cha ACT-Wazalendo, kimemuandikia barua Spika wa Bunge, Job Ndugai  kikimuomba kufanya uchunguzi maalumu kuhusu kiasi cha Sh1.5 trilioni ambazo hazionekani kwa mujibu wa taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti  Mkuu wa Hesabu  za  Serikali (CAG).

Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mawasiliano kwa Umma wa ACT-Wazalendo, Ado Shaibu amesema hayo leo Alhamisi Aprili 19, 2018 wakati akizungumza  na waandishi  wa habari kuhusu ufafanuzi wa kauli  na hoja zilizosemwa na CCM jana.

"Sasa hivi CCM wakithubutu kutochokoza ACT-Wazalendo, swali letu ni moja tu Sh 1.5 trilioni ziko wapi? Upinzani tuna wajibu wa kuhoji ili kuhakikisha  Watanzania wanajua fedha zao zinakwenda wapi," amesema.

Shaibu amesema barua hiyo imeandikwa na Mwenyekiti  wa Chama hicho, Jeremiah Maganja akimuomba Ndugai kutoa kibali maalumu kwa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), ikutane na imuagize CAG kufanya ukaguzi kuhusu fedha ili zijulikane zilizokopelekwa.

"Matumaini yetu Spika Ndugai atazingatia maombi haya. Lengo letu Watanzania  wajue ukweli kwa sababu  kumekuwa na upotoshaji mkubwa ukiendelea kuhusu fedha hizi," amesema Shaibu.

Amesema chama hicho hakitarudi nyuma katika sakata hilo na kuwaomba Watanzania kuwaunga mkono hadi hatua ya mwisho ili kujua ziko wapi kwa sababu ni fedha nyingi.