VIDEO: Nassari afunguka ushuru wa korosho

Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari akichangia mjadala wa kupitisha Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2018/2019, jijini Dodoma leo. Picha na Edwin Mjwahuzi

Muktasari:

Asema fedha kutotolewa 

Dodoma. Mbunge wa Arumeru Mashariki ( Chadema),  Joshua Nassari amekifananisha na wizi kitendo cha Serikali kushindwa kutoa Sh 210 bilioni kama asilimia 65 ya fedha za ushuru wa mauzo ya korosho nje ya nchi kwa kuwa jambo hilo lipo kisheria.

Akizungumza katika mjadala wa bajeti ya Serikali mwaka 2018/19 leo Juni 25, 2018 bungeni mjini Dodoma, Nassari amesema asilimia kubwa ya wabunge bungeni wanawawakilisha wakulima, wafugaji na wavuvi.

Amesema hata dhana ya Tanzania ya viwanda inategemea malighafi za kutosha zinazotokana na zao hilo lakini bajeti imekuwa ikipungua mwaka hadi mwaka.

Amesema shughuli za kilimo cha korosho sasa zimepanuka na wakulima katika mikoa 17 sasa wanalima zao hilo la biashara lakini Serikali haitaki kutoa fedha hizo ambazo wakulima wamekuwa wakizitegemea.

Amesema kama Serikali ilitunga sheria ya korosho iweje sasa itake kuibadilisha ili fedha hizo ziende katika Mfuko wa Hazina.