Vigogo 11 CCM kuenguliwa mabadiliko ya CCM

Muktasari:

CCM inatarajia kupitisha mabadiliko makubwa ya katiba, ambayo yatapunguza idadi ya wajumbe katika vikao vya juu na pia kupunguza kofia za uongozi mwanachama mwenye cheo ndani ya chama, ubunge au serikalini.


Dar es Salaam/Dodoma. Wakati mabadiliko ya katiba yatawaengua vigogo 11 katika uongozi wa CCM walio na kofia zaidi ya moja, hatima ya idadi kama hiyo ya wanachama wanaodaiwa kukisaliti chama hicho wakati wa Uchaguzi Mkuu uliopita, itajulikana kesho.

CCM inatarajia kupitisha mabadiliko makubwa ya katiba, ambayo yatapunguza idadi ya wajumbe katika vikao vya juu na pia kupunguza kofia za uongozi mwanachama mwenye cheo ndani ya chama, ubunge au serikalini.

Mabadiliko hayo yalipendekezwa na Halmashauri Kuu ya CCM, iliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam Desemba 13 mwaka jana.

Mabadiliko hayo yalitangazwa kwenye vyombo vya habari na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM aliyemaliza muda wake, Nape Nnauye kwamba muundo wa chama umebadilika na mwanachama anatakiwa kuwa na nafasi moja tu ya uongozi wa kazi za muda wote kama ilivyoainishwa kwenye Kanuni za Uchaguzi wa CCM, Toleo la 2012, Kifungu cha 22 na 23.

Nape alizitaja nafasi hizo kuwa ni mwenyekiti wa tawi, kijiji au mtaa, kata/wadi, jimbo, wilaya na mkoa. Wengine ni makatibu wa halmashauri kuu wa ngazi zote, mbunge, mwakilishi na diwani.

Mabadiliko hayo pia yamepunguza ukubwa wa Kamati Kuu kutoka wajumbe 34 hadi 24, hali inayofanya wanaoingia kwa kupigiwa kura kupungua hadi wanne kutoka kumi.

Pia nafasi za ujumbe wa Halmashauri Kuu zimepungua kutoka 388 hadi 158, huku wengi wakiingia kwa nafasi zao na wajumbe kutoka wilayani kuondolewa.

Kutokana na mabadiliko hayo, baadhi ya viongozi wenye kofia zaidi ya moja wameshaanza kutangaza kutotetea nafasi zao katika uchaguzi ujao wa viongozi wa CCM na jumuiya zake.

Wa kwanza alikuwa Sophia Simba ambaye ni mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake (UWT) Sophia Simba. Simba pia mbunge na mjumbe wa Kamati Kuu.

Mwingine ni Abdallah Bulembo aliyetangaza kuwa hatagombea uenyekiti wa Umoja wa Wazazi wa CCM. Bulembo ameteuliwa na Rais Rais John Magufuli kuwa mbunge, jambo linalomfanya awe na kofia mbili.

Mbali na hao waliotangaza hadharani, wapo vigogo wengine ambao wana nafasi zaidi ya moja za uongozi, akiwamo Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Hussein Mwinyi ambaye mbali na uwaziri ni mbunge, mjumbe wa NEC na mjumbe wa Kamati Kuu.

Pia Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi ni mbunge na mjumbe wa Kamati Kuu, kama ilivyo kwa Profesa Makame Mbarawa (Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano) ambaye ni mjumbe wa Kamati Kuu wakati Shamsi Vuai Nahodha ni mbunge na mjumbe wa Kamati Kuu.

Mabadiliko hayo pia, yatawakumba wenyeviti wa CCM wa mikoa ambao kwa nafasi zao ni wajumbe wa NEC. Mmojawapo ni Kimbisa, ambaye ni mwenyekiti wa Mkoa wa Dodoma na mjumbe wa Kamati Kuu.

Wenyeviti wa mikoa ambao pia ni wabunge ni Joseph Msukuma (Geita), Martha Mlata (Singida) na Deo Simba (Njombe). Mwenyekiti wa CCM wa Mbeya, Godfrey Zambi pia ni mjumbe wa NEC na mkuu wa Mkoa wa Lindi.

Mwingine anaonekana kuguswa na mabadiliko hayo ni Salma Kikwete ambaye ni mjumbe wa NEC anayewakilisha Wilaya ya Lindi Mjini na ambaye hivi karibuni aliteuliwa na Rais kuwa mbunge.

 

Maoni ya CCM, Mbunge Njombe

Alipoulizwa kuhusu mabadiliko hayo, naibu katibu mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai alisema suala la kofia mbili litajadiliwa na kutolewa uamuzi na Halmashauri Kuu.

“Tusiwahishe ajenda hiyo. Hatuzuii mtu kujiuzulu kwa utashi wake, lakini jambo hilo litajadiliwa na Kamati Kuu na mwishowe kwenye Halmashauri Kuu chama kitaweka wazi nini kitafanyika kwa sababu huko ndipo yatangazwa mabadiliko ya kanuni na ratiba ya uchaguzi ndani ya chama utakavyokuwa kuanzia ngazi ya matawi,” alisema Vuai.

Mbunge wa Njombe Kaskazini, Deo Sanga ni miongoni mwa wanachama wenye kofia mbili, akiwa pia mwenyekiti wa CCM wa Mkoa wa Njombe. Alipoulizwa atavua kofia gani kati ya ubunge na uenyekiti, alisema anasubiri mwongozo wa Halmashauri Kuu.

“ Mimi ni mjumbe natarajia kwenda huko huko. Mwongozo ukitolewa ndipo nitajua cha kufanya, lakini kwa sasa siwezi kukueleza kwa uhakika,” alisema Sanga.

Wengine waliotafutwa kuzungumzia suala hilo hawakupatikana, isipokuwa Msukuma ambaye alisema yuko kikaoni.

 

Hatua kali za kinidhamu

Lakini hoja inayotarajiwa kutingisha ni ya kujadili mchakato wa uteuzi wa wagombea wa CCM na mambo yaliyojitokeza katika kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.

Miongoni mwa wanachama watakaokuwa katika wakati mgumu ni wajumbe watatu wa Kamati Kuu ambao walipinga hadharani maamuzi ya chombo hicho ya kupitisha majina matano ya wagombea urais kwa maelezo kuwa katiba ya CCM ilikiukwa.

Wajumbe hao ni Sophia Simba, Adam Kimbisa na Emmanuel Nchimbi.

Waliopitishwa walikuwa Bernard Membe, January Makamba, Dk Asha-Rose Migiro, Balozi Amina Salum Ali na John Magufuli (ambaye alishinda na sasa ndiye Rais).

Chanzo cha habari kililiambia Mwananchi kuwa baadhi ya wanachama hao wameshahojiwa na Kamati ya Maadili na kwamba kinachosubiriwa sasa ni uamuzi.

“Kamati ya maadili imeshamuhoji Sophia Simba na wanachama wengine na NEC inakaa na kupokea mapendekezo ya Kamati ya Maadili, hapo ndiyo hatma yao itajulikana. Lakini nakwambia ndugu yangu hawa watu sasa hawawezi kutoka,” alisisitiza.

Mwananchi ilipomtafuta Simba kuhusu suala hilo alisema hayo ni maneno ya mtaani na kwamba chama kina taratibu zake.

“Chama kina taratibu zake hakiwezi kuyumbishwa na maneno ya mitaani. CCM ina taratibu zake na maamuzi yanapitia vikao halali vya chama,” alisema Simba.

“Kwanini unataka tuvuke mto ilihali hatujafika.”

Alipoulizwa kuhusu taarifa kuwa alihojiwa pamoja na watuhumiwa wengine, alisema hizo ni taratibu za kawaida katika chama chao.

“Ninachofahamu kuhojiwa ni taraibu za kawaida sina kesi yoyote,” alisema.

Juhudi za Mwananchi hazikufanikisha kumpata Kimbisa, hali kadhalika Nchimbi ambaye kwa sasa ameteuliwa kuwa balozi nchini Brazil kutokana na simu zao kutopatikana.

Wengine watakaokuwa katika wakati mgumu ni wanachama wanaodaiwa kukisaliti chama wakati wa kampeni za uchaguzi na ambao walijadiliwa kuanzia ngazi ya wilaya na baadaye mapendekezo kuwasilishwa vikao vya juu na baadaye Kikwete kumkabidhi Rais Magufuli ripoti hiyo.

Mara kadhaa viongozi wa chama hicho walikaririwa wakitaka wasaliti wa chama kuchukuliwa hatua, akiwamo Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan ambaye aliwataka viongozi wa CCM wa Mkoa wa Kaskazini A kisiwani Unguja kuwachukulia hatua zinazostahili wanachama wanaokisaliti na kukihujumu chama.

Pia, mara kadhaa wakati wa kampeni, Rais Magufuli alikuwa akituhumu wanachama kuwa walikuwa wakionyesha kuwa CCM mchana na usiku wakipigia kampeni wagombea wa vyama vilivyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).

Katika uchaguzi huo, vyama vya upinzani viliendelea kuipokonya CCM viti huku mgombea urais aliyeungwa mkono na Ukawa, Edward Lowassa akipata takriban asilimia 40 ya kura zote, ikiwa ni mara ya kwanza tangu uchaguzi wa vyama vingi urudishwe mwaka 1995.

Wanachama wanaodaiwa kukisaliti chama hicho ni pamoja na mwenyekiti wa CCM wa Mkoa wa Iringa, Jesca Msambatavangu, ambaye amekuwa akilalamikiwa kutokana na CCM kufanya vibaya katika uchaguzi wa jimbo la Iringa Mjini lililochukuliwa tena na Mchungaji Peter Msigwa wa Chadema.

 

Bulembo ajiuzulu

Katika hatua nyingine, jana katika kikao cha Baraza Kuu Maalum la Jumuiya ya Wazazi, Bulembo alitangaza kutotetea nafasi yake ya unyekiti.

“Kila mmoja ni shahidi, wakati naingia, jumuiya hii ilikuwa inakwenda kufa, jambo lililosababisha aliyekuwa mwenyekiti wa CCM, Jakaya Kikwete kutaka kuifuta. Lakini nikamuhakikishia ataona mapinduzi akiniachia,” alisema Bulembo.

“Sasa natoka kifua mbele, yale yote niliyoyaahidi nimetimiza kwa asilimia 75. Tangu nimeingia hatujawahi kuomba hata shilingi moja kwa ajili ya uendeshaji,” alisema.

Hata hivyo, Bulembo alisema ataendelea na vikao vyote mpaka Oktoba atakapomkabidhi rasmi mwenyekiti mpya.

Alisema kwa sasa asiulizwe kwa nini amechukua uamuzi huo na kwamba hoja siyo kuteuliwa kwake kuwa mbunge bali ni utaratibu aliojiwekea katika maisha yake.