Viongozi Chaumma waungana na JPM kuhamia Dodoma

Rais John Magufuli

Muktasari:

Makamu Mwenyekiti wa chama hicho Kayumbo Katubali alisema ujio wa Serikali bado ni wa kusuasua kuliko kama Chaumma kingeingia madarakani kwani kilikuwa na mkakati thabiti wa kuanzia Serikali yao Dodoma tangu siku ya kiapo.

Dodoma. Chama cha Ukombozi wa Umma (Chaumma) kimempongeza Rais John Magufuli kwa hatua yake ya kutekeleza azimio la kuhamishia makao makuu ya Serikali mkoani Dodoma, huku kikisema huo ndiyo ulikuwa mkakati wa chama hicho wa muda mrefu.

Makamu Mwenyekiti wa chama hicho Kayumbo Katubali alisema ujio wa Serikali bado ni wa kusuasua kuliko kama Chaumma kingeingia madarakani kwani kilikuwa na mkakati thabiti wa kuanzia Serikali yao Dodoma tangu siku ya kiapo.

“Nampongeza Magufuli, ametuonyesha kwa vitendo siyo maneno yaliyokuwa yakisemwa na wanachama wa chama chake kwa zaidi ya miaka 40. Sisi kwenye ilani yetu ya Uchaguzi Mkuu tulipanga kuanzia Dodoma na si vinginevyo,” alisema Kabutali.

Kabutali alisema kwenye ilani yao ya uchaguzi, ibara ya 18 walieleza Serikali yao itakuwa Dodoma baada ya kutangazwa washindi. Mwanasiasa huyo alimtaka Rais Magufuli kukamilisha mchakato wa kuhamia mjini hapa kwa kuutungia sheria ili wanasiasa wasitoe matamko yasiyo na tija.

Kuhusu wakazi wa Dodoma alisema kuwa huenda ikawa faraja kwao kwani kwa sasa Serikali itakuwa karibu nao hivyo watapumzika manyanyaso waliyokuwa wakiyaopata wanapotafuta ardhi.

Alisema wakazi wa Dodoma walishachoshwa na urasimu wa Mamlaka ya Uendelezaji Makao Makuu (CDA) na ndiyo maana migogoro ya ardhi ikawa haimaliziki. Aliwataka wana-Dodoma wawe makini na wasikubali kudanganywa na wajanja katika masuala ya ardhi.