Viwanja, mashamba ya Musukuma kupigwa mnada

Mbunge wa Geita Mjini, Joseph Kasheku maarufu kama Musukuma

Muktasari:

Mali zinazopigwa mnada ni kiwanja cha Mbezi na cha Korogwe Mjini. 

Dar es Salaam. Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) kupitia kampuni ya udalali ya LJ International Ltd imetangaza kuzipiga mnada mali za Mbunge wa Geita vijijini, Joseph Kasheku maarufu kama Musukuma.

Mali zilizotajwa kupigwa mnada  ni pamoja na kiwanja Na.275 Block kilichopo Mbezi Dar es Salaam na kiwanja Na.’2’ block ‘A’kilichopo Korogwe mjini.

Mali nyingine ni shamba Na.201 liliolopo kijiji cha Igate Mkoani Geita, kiwanja Na. 116 block A Buswelu Kaskazini na kiwanja Na. 48 block T katikati ya jiji la Mwanza.

 Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Benki ya NBC, William Kalage amesema ni kweli  mali hizo zinapigwa mnada.

“Ni kweli tumetoa tangazo na sisi ndiyo tumeipa kazi hiyo kampuni ya udalali kupiga mnada mali hizo,” amesema

Mbali na Musukuma, kampuni ya LJ International Ltd pia imetangaza watu 19 wanaodaiwa na benki hiyo ambao mali zao zitanadiwa.

Hata hivyo Musukuma hakupatikana kwa njia ya simu kuzungumzia suala hilo. Hivi karibuni mwanasiasa huyo amekuwa akimpigia kampeni mgombea ubunge wa jimbo la Monduli kwa tiketi ya CCM, Julius Kalanga.