Waafrika 200 waliofungwa Israel kuachiwa

Muktasari:

Israel imekuwa ikijaribu kufikia makubaliano na Uganda kuwachukua wahamiaji hao walioingia nchini humo kwa miguu kupitia mpaka wa Misri muongo mmoja uliopita.

Jerusalem, Israel. Serikali ya Israel imesema itawaachilia huru wahamiaji wa Kiafrika 200 ambao wamefungwa katika gereza la Jangwani nchini humo.

Israel imekuwa ikijaribu kufikia makubaliano na Uganda kuwachukua wahamiaji hao walioingia nchini humo kwa miguu kupitia mpaka wa Misri muongo mmoja uliopita.

Wafungwa hao wanaotarajiwa kuachiliwa huru, walipelekwa katika gereza la Jangwani katika miezi ya hivi karibuni kusubiri safari ya kupelekwa nchini Uganda.

Serikali ya Israel imesema wahamiaji 37,000 waliopo nchini humo wanatafuta kazi na kwamba, ina kila haki ya kulinda mipaka yake.

Wahamiaji hao pamoja na makundi ya kutetea haki za binadamu wanasema wako hapo kutafuta hifadhi na wanakimbia vita na unyanyasaji nchini mwao.