Wabunge wa Congress wataka Marekani isaidie suluhu Liberia

Muktasari:

Katika barua ambayo gazeti la FrontPageAfrica lilipata nakala yake, watunga sheria hao wa Marekani wameonyesha masikitiko yao kuhusu uwezekano wa shauri kuchukua muda mrefu na mgawanyiko katika mchakato wa kidemokrasia.

 

Monrovia, Liberia. Baadhi ya wajumbe wa Baraza la Congress la Marekani wamesema kuwa amani na utulivu viko hatarini; siyo Liberia tu, bali pia ukanda wote wa Afrika Magharibi.

Wabunge Sheila Johnson Lee na Bobby L. Rush waliguswa na mkwamo wa kisiasa nchini Liberia uliosababishwa na madai ya udanganyifu na dosari katika uchaguzi mkuu wa rais na wabunge uliofanyika Oktoba 10.

Watunga sheria hao wa Congress wamemwandikia barua Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Rex Tillerson wakiitaka Serikali ya Marekani ifanye haraka kuingilia mambo yalivyo Liberia ili kuhakikisha madai ya udanganyifu katika kura yanashughulikiwa haraka kuepuka usijitokeze mgogoro wa kikatiba.

Katika barua ambayo gazeti la FrontPageAfrica lilipata nakala yake, watunga sheria hao wa Marekani wameonyesha masikitiko yao kuhusu uwezekano wa shauri kuchukua muda mrefu na mgawanyiko katika mchakato wa kidemokrasia.

Walifurahishwa na namna vyma vya siasa vyenye malalamiko vilivyoanzisha mchakato wa kisheria kupata haki na wakapongeza vyama hivyo kuzingatia utawala wa kisheria, lakini wameitaka serikali ya Marekani kuhimiza na kuunga mkono juhudi za kupata ufumbuzi haraka.

Wasiwasi wao kuhusu mgawanyiko ni kwamba unaweza usiishie Liberia tu kwani wanaamini ikiwa mkwamo wa kisiasa hautapata suluhu haraka unaweza kusambaa na kusababisha ukosefu wa utulivu kwa eneo lote na hivyo kuvuruga mchakato wa amani uliofikiwa