Wabunge wabana matumizi, wachangia madarasa

Muktasari:

Wabunge hao ni wa Maswa Mashariki na Magharibi mkoani Simiyu wamechangia mabati 3,750 yenye thamani ya Sh68 milioni kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa vyumba 130 vya madarasa.

Maswa. Ikiwa kazi yao kubwa ni kuhamasisha na kuchangia maendeleo kupitia kwa wapigakura wao, wabunge wa Wilaya ya Maswa wamechangia mabati ya ujenzi wa madarasa.

Wabunge hao ni wa Maswa Mashariki na Magharibi mkoani Simiyu wamechangia mabati 3,750 yenye thamani ya Sh68 milioni kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa vyumba 130 vya madarasa.

Pia, wamekabidhi madawati 1,074 yaliyotengenezwa na fedha zilizopatikana baada ya kubana matumizi huku kila jimbo likipata madawati 537.

 Makabidhiano ya  mabati na madawati hayo yamefanyika katika viwanja vya Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Maswa na kuhudhuriwa na wananchi na Mkuu wa wilaya hiyo, Dk Seif Shekalaghe.

Mbunge wa Maswa Mashariki, Stanslaus Nyongo amesema fedha zilizonunua mabati hayo zimetoka Mfuko wa Maendeleo wa majimbo hayo.

Naye Mbunge wa Maswa Magharibi, Mashimba Ndaki amesema wamechukua uamuzi huo ili kuwapunguzia wananchi mzigo wa kuchangia gharama za kujenga miundombinu ya elimu shuleni.