Wadau wazungumzia mambo sita ya waraka

DR. SHOO: HATUTAKUBALI KUNYAMAZISHWA, JUKUMU LETU KUONYA

Muktasari:

Taasisi hizo zimeishauri Serikali kuyatafutia ufumbuzi masuala hayo ili kuleta usawa katika jamii.


Dar es Salaam. Tangu kuanza kwa mwaka huu, kumekuwa na mijadala, matamko na hata baadhi ya taasisi kutoa waraka jinsi mambo yanavyoendelea nchini.

Hata hivyo, si mara ya kwanza kuwapo kwa mijadala ya aina hiyo nchini, lakini safari hii mambo sita yamekuwa yakijirudia mara kwa mara ambayo yamezungumziwa na wadau kwa mitazamo tofauti.

Madai ya Katiba Mpya; kuingiliwa Bunge na Mahakama kiutendaji; mikutano ya siasa kuzuiwa; kuminywa vyombo vya habari; hali ya uchumi nchini; na uhuru wa kutoa maoni ndiyo mambo yanayozua mjadala zaidi miongoni mwa yaliyojitokeza.

Hili linajidhihirisha kutokana na mambo hayo kuwamo katika waraka au matamko yaliyotolewa kwa nyakati tofauti kuanzia Februari kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) na Baraza la Maaskofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT).

Taasisi hizo zimeishauri Serikali kuyatafutia ufumbuzi masuala hayo ili kuleta usawa katika jamii.

Februari 11, TEC ilitoa ujumbe wa Kwaresima wa mwaka 2018 huku maaskofu wake wakitoa maoni kuhusu masuala ya kisiasa, kiuchumi na kijamii.

Mwishoni mwa wiki iliyopita, KKKT pia walitoa ujumbe wa Sikukuu ya Pasaka uliosainiwa na maaskofu 27 ambao licha ya kuzungumzia masuala ya kiroho, ulitaja changamoto hizo tatu.

Februari 21, TCD iliandaa kongamano la viongozi wa siasa na dini lililoazimia kuonana na Rais John Magufuli ambalo pia lilipendekeza kukamilishwa kwa mchakato wa kupatikana kwa Katiba Mpya.

Katika pendekezo jingine, TCD ilieleza umuhimu wa kujengwa taasisi imara za usawa na haki.

Kauli za wachambuzi

Baadhi ya wachambuzi wa masuala ya kisiasa na haki za binadamu waliotakiwa kutoa maoni yao kuhusu mambo hayo sita kujadiliwa zaidi wameishauri Serikali kuyafanyia kazi kwa kuwa yanaonyesha hali halisi ya nchi ilivyo.

Profesa wa Chuo Kikuu Katoliki cha Ruaha (Ruco), Gaudence Mpangala alisema, “Nimemaliza kupitia waraka wa KKKT na ule wa TEC nikichanganya na wa asasi mbalimbali, naona wanazungumza hali halisi ya Tanzania ya sasa na mustakabali wa ujenzi wa maendeleo.

“Sielewi, wasiwasi wangu ni je, Serikali inayachukulia maanani haya matamshi yote. Tangu lilipotolewa tamko la maaskofu wa Katoliki wiki kama tano zilizopita kila nikiangalia sioni mabadiliko. Ukijiuliza kwa nini hata Katiba ya sasa ..... hupati jibu.”

Profesa Mpangala anaungwa mkono na mkurugenzi mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Hellen Kijo-Bisimba aliyesema, “Inatuonyesha hali halisi ya nchi yetu, ukigeuka mbele au nyuma unayaona.

“Ninachofikiri utawala uliopo madarakani ungekaa chini na kuyaona haya na kubadili hali kwa kuwa kila waraka unatoka na mapendekezo. Sauti zimekuwa nyingi,” alisema.

Dk Kijo-Bisimba alisema viongozi wa kiroho wanazungumza kwa lugha nyepesi, hivyo itumike kutafakari na kusikia kile wananchi wanachokitaka.

“Serikali inapaswa kuangalia kipaumbele cha wananchi, kipaumbele cha Serikali ni watu waliowaweka madarakani na wananchi wanahitaji Katiba Mpya hivyo Serikali inapaswa kusikia,” alisema Dk Kijo-Bisimba.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Richard Mbunda alisema, “Haya matamko yanagusa siasa, tungekuwa tunayasikia katika majukwaa ya siasa, wanasiasa wenyewe au yangezungumzwa bungeni lakini kwa sababu huko majukwaani hakuna nafasi ya ushiriki ndiyo maana wamekuja wao na kuyazungumza,” alisema.

“Matamko yanatolewa kama ushauri, ni jukumu la Serikali kuangalia na kuchuja kisha kuyafanyia kazi si kupuuza, taasisi hizi za kidini ukiangalia kama DRC (Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo) maandamano yanaitishwa na taasisi za kidini kitu ambacho hakikuwapo. Kwa hiyo, ushauri unaotolewa ufanyiwe kazi isije kujitokeza kwetu.”

Kilichomo katika matamko

Ujumbe wa TEC uliotolewa wiki moja kabla ya kuanza Kwaresima ulieleza uamuzi wa Serikali kuzuia maandamano, mikutano ya hadhara, makongamano na mijadala ya siasa ni kwenda kinyume cha Katiba ya nchi.

Pia, ujumbe huo ulionya hatua ya Serikali kuvibana vyombo vya habari ikiwa pamoja na kuvifungia kwa sababu mbalimbali, kuingiliwa kwa Bunge na Mahakama kwamba hatua hiyo itajenga chuki kiasi cha kuhatarisha amani ya nchi, usalama na hadhi ya binadamu.

TEC imesema ina wajibu wa kuhakikisha maisha ya walio wanyonge, maskini na walio pembezoni mwa jamii wanapata unafuu.

Ujumbe wa TEC unashabihiana na wa KKKT ambao maaskofu wake wakiongozwa na mkuu wa kanisa hilo, Dk Frederick Shoo wameutoa ukiwa mahsusi wa salamu za Sikukuu ya Pasaka ukiwa na jina “Taifa letu amani yetu” ukigusia hali ya kijamii na kiuchumi, maisha ya siasa na masuala mtambuka likiwamo la Katiba Mpya.

Maaskofu wa KKKT katika tamko hilo wanasema, “Kwa umoja wetu katika utume, tunatambua siasa safi na uongozi bora ni misingi iliyoongoza maisha ya siasa katika Taifa letu.

“Taifa huongozwa na Katiba iliyo kiini cha sheria zote. Taifa haliongozwi na ilani za vyama. Serikali huongozwa na Katiba, sheria, kanuni na mapokeo mema (misingi na tunu za Taifa). Serikali husimamiwa na Bunge huru lililo sauti ya wananchi.”