Wafanyabiashara manusura kuchoma kituo cha zima moto

Kamanda wa Polisi mkoani Shinyanga, Jumanne Mliro alisema tukio amelisikia lakini taarifa hajapata watafanya uchunguzi ili kubaini chanzo chake

Muktasari:

  • Tukio hilo limetokea leo mchana baada ya mwananchi huyo kudaiwa kuzimia kwa kupigwa na askari hao na kutaka kukichoma moto kituo hicho wakidai kitendo hicho siyo cha kiungwana.

Shinyanga. Wafanyabiashara katika soko la nguzo nane Kata ya Kambarage Manispaa ya Shinyanga, wamevamia kituo cha jeshi la zimamoto kilichopo katika maeneo ya soko hilo  baada ya askari wa jeshi hilo kumpiga mwananchi aliyepita karibu na ofisi hiyo.

Tukio hilo limetokea leo mchana baada ya mwananchi huyo kudaiwa kuzimia kwa kupigwa na askari hao na kutaka kukichoma moto kituo hicho wakidai kitendo hicho siyo cha kiungwana.

Baadhi ya wananchi walioshuhudia tukio hilo akiwemo Josephat Musa na Janeth Magayane walikilalamikia kituo hicho kwa kuwapiga mara kwa mara wananchi wanaopita karibu ya kituo hicho licha ya kituo hicho kutokuwa na uzio.

Kwa upande wake diwani wa kata hiyo Kambarage Mwendapole alisema baada ya kufika eneo hilo alikuta wananchi wamezingira katika kituo cha zimamoto wengine wakiponda mawe kwenye magari na wengine wakitaka kuchoma magari na jengo, ambapo aliwaomba wawe watulivu ili waje polisi wamchukue mwananchi aliyepigwa.

Kaimu kamanda wa zimamoto mkoa, Edward Lukuba alisema katika kituo hicho hawaruhusiwi wananchi kupenyeza pembeni, badala yake wapite getini “naona aliwajibu vibaya baada ya kupita sehemu inayokatazwa,"

Kamanda wa Polisi mkoani Shinyanga, Jumanne Mliro alisema tukio amelisikia lakini taarifa hajapata watafanya uchunguzi ili kubaini chanzo chake