Wafuasi wa Lipumba wakusanyika Buguruni kumwingiza ofisini

Muktasari:

Wanachama hao wanadai wana barua ya Msajili wa vyama vya siasa inayomtambua Profesa Lipumba kama mwenyekiti halali wa CUF.

Dar es Salaam. Vikundi vya wafuasi Profesa Ibrahim Lipumba wamekusanyika katika Ofisi za CUF Buguruni wakisubiri kumpokea mwenyekiti huyo wa zamani na kumwingiza ofisini.

Wanachama hao wanadai wana barua ya Msajili wa vyama vya siasa inayomtambua Profesa Lipumba kama mwenyekiti halali wa CUF.

Mwandishi wa Mwananchi, Ephrahim Bahemu aliyeko kwenye eneo hilo anasema geti la ofisi za CUF limefungwa na ndani hakuna kiongozi yeyote wa chama.

Bahemu anasema mashabiki hao wa Lipumba wanaoimba na kucheza, wanasema msafara wa Profesa uko njiani kuelekea kwenye ofisi hizo za makao makuu ya chama hicho.

Alipoulizwa kuhusu hali hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi ya CUF, Julius Mtatiro amesema ndio wamepokea barua ya msajili na bado wanaisoma ili kuona imeelekeza kitu gani.

Hata hivyo, Mtatiro amesema kwa vyovyote vile msajili wa vyama vya siasa hana mamlaka ya kuingilia maamuzi ya vikao vya chama chochote cha siasa.