Wajasiriamali, wadau wa biashara wakutana UDSM

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Rwekaza Mukandala 

Dar es Salaam. Wajasiriamali, watalaamu na wadau wa biashara wamekutana kwa ajili ya kujadili namna ya kuwazesha wafanyabiashara wa kati, wakubwa na wadogo ili kukuza biashara zao zitakazosaidia kuongeza pato la Taifa.

Wajasiriamali na wadau wamekutana leo Alhamisi katika mkutano wa 17 wa wajasiriamali uliondaliwa na Shule Kuu ya Biashara ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDBS).

Akifungua mkutano huo, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Rwekaza Mukandala alisema mkutano huo ni muhimu kwa wajasiriamali na ni miongoni mwa juhudi zinazofanywa na katika kuwasidia wafanyabiashara wa kubwa, wa kati na wadogo ili kuijenga Tanzania ya viwanda.

"Lengo na mkutano huu wa 17 ni kuwasidia wafanyabiashara na wajasiriamali mbinu za kufanikiwa katika shughuli zao. Kuna vikwazo vingi wanakutana navyo ikiwamo mtaji mdogo  na mazingira yasiyo rafiki kwao,"alisema Profesa Mukandala.

Alisema mkutano ni wa siku mbili  na baada ya majadiliano washiriki watatoka na maazimio na yatakayokuwa chachu ya kukuza biashara zao kwa wafanyabiashara na wajasiriamali na yatasambazwa kwao kupitia njia mbalimbali ikiwamo vyombo vya habari.

Mkuu wa shule hiyo, Dk Ulingeta Mbamba alisema zaidi ya mada 50 zitwasilishwa kutoka kwa washiriki mbalimbali wa ndani ya nchi na nchi za  nje nane  zikiwamo za Afrika Mashariki.

Mbali na hilo, Dk Mbamba alisema shule hiyo itaendelea  kutoa elimu kwa wajasiriamali wa dogo, wakubwa na wakati sanjari na kuwatafutia mbinu za kutafuta masoko na namna ya kutunza fedha zao.

Mkuu wa Taasisi  Kuendeleza Sekta za Fedha (FSDT), Peter Kingu alisema mkutano huo utasaidia pia kubadilishana kuhusu ujasiriamali  miongoni wa washiriki kwa kuwa baadhi ya wamefanya tafiti mbalimbali .