Wakili wa Maua Sama awasilisha ombi la dhamana mahakamani

Muktasari:

Wakili Jebra Kambole amewasilisha maombi Mahakama ya Kisutu akitaka wateja wake Maua Sama, meneja wake Fadhili Kondo na mtangazaji wa kipindi cha Shilawadu,  Soudy Brown wanaoshikiliwa kituo kikuu cha polisi kwa siku tano,  kupewa dhamana

Dar es Salaam. Wakati mwanamuziki Maua Sama, meneja wake Fadhili Kondo na mtangazaji Soudy Brown wakiendelea kusota rumande, wakili wao Jebra Kambole amewasilisha maombi Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, akitaka wateja wake kupewa dhamana.

Akizungumza na MCL Digital leo Ijumaa Septemba 21, 2018 Kambole amesema kwa hatua za awali tayari wamewasilisha maombi ya dhamana ili wateja wake wanaoshikiliwa kwa makosa ya mtandao waweze kuachiwa kwa dhamana kwa kuwa wanashikiliwa kwa takribani siku tano.

“Tayari tumewasilisha maombi Mahakama ya Kisutu kutaka wateja wetu wanaoishikiliwa kwa siku tano wapewe dhamana. Polisi wao waendelee kukamilisha upelelezi wao wakati wateja wangu wakiwa nje kwa dhamana,” amesema Kambole.

Amesema sheria iko wazi, inaeleza ni muda gani polisi inapaswa kukaa na mtuhumiwa, kama wanataka kuendelea na uchunguzi wanaweza kufanya hivyo mhusika akiwa nje kwa dhamana.

Wateja hao wa Kambole pamoja na mtangazaji wa Clouds, Shaffi Dauda , msemaji wa Chadema, Tumaini Makene na watuhumiwa wengine watano wanashikiliwa na polisi kwa kosa la mtandao.

Septemba 16, 2018 Maua, Soudy na Fadhili walikamatwa na polisi baada ya video iliyokuwa ikisambaa katika mitandao ya kijamii kuwaonyesha wakirusha hela na kujikanyaga.

Dauda na mshehereshaji Athony Luvanda wanashikiliwa kwa madai ya kumiliki mtandao wa Youtube na maudhui yake kinyume na sheria.