Wanandoa wachomana visu wakiwa ‘gesti’ ya Enjoy

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi 

Muktasari:

Tukio hilo limetokea leo alfajiri Juni 19 saa 11:00 asubuhi 

Sengerema. Michael Daudi (31) Mkazi wa kijiji na Kata ya Bukokwa Halmashauri ya Buchosa wilayani hapa Mkoa wa Mwanza, amemuua mke wake Tekla Lutandula (30) kwa kumchoma visu sehemu mbalimbali za mwili wake kisha naye kujiua kwa kujichoma visu tumboni.

Tukio hilo limetokea leo alfajiri Juni 19 saa 11:00 asubuhi wakati wamelala nyumba ya wageni iitwayo Enjoy katika Kijiji cha Kanyala Kata ya Bulyaheke wilayani Sengerema.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi amethibisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba chanzo chake ni wivu wa kimapenzi.

Ofisa Mtendaji wa Kata ya Bulyaheke, Musa Mwilomba alisema Tekla kwa sasa alikuwa akiishi katika Kijiji cha Kanyala na kwamba Daudi alimchoma Tekla visu 11 kisha na yeye kujichoma visu saba.

Mama mzazi wa Tekla, Devotha Shadrack amesema wanandoa hao walikuwa na ugomvi wa kifamilia na walishauriwa na kufikia muafaka  na mwanaye alikuwa naye nyumbani kwao (kwa mama).

“Sikujua chochote kama mwanangu amelala gesti nimeshangaa kupata taarifa za mwanagu kuuawa,” amesema.

Mmoja wa wananchi waliokuwa wamelala ndani ya nyumba ya wageni aliyejitambulisha kwa jina moja la Magret alisema walisikia kelele lakini mwanaume huyo amedai atakayesogea atauawa.