Wanawake 600 wakopeshwa Sh120 milioni bila riba Arusha

Muktasari:

  • Fedha hizo zimetolewa na ofisi ya mkuu wa Mkoa wa Arusha akisaidiana na jumuiya ya wafanyabiashara Arusha, katika mkakati wa kusaidia makundi maalumu wakiwamo walemavu na wanawake.

 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, anayeshughulikia ajira, Jenista Mhagama jana aliwakabidhi wanawake 600 wakazi wa Arusha, hundi ya Sh120 milioni ikiwa ni mkopo usio na riba.

Fedha hizo zimetolewa na ofisi ya mkuu wa Mkoa wa Arusha akisaidiana na jumuiya ya wafanyabiashara Arusha, katika mkakati wa kusaidia makundi maalumu wakiwamo walemavu na wanawake.

Katika fedha hizo kila mwanamke atapokea mkopo wa Sh200,000.

“Naamini utawasaidia mliokopeshwa mtarejesha kwa wakati,” alisema Mhagama.

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi na Ajira), Anthony Mavunde alisema “Fedha ya leo iwe mbegu inayokwenda kubadilisha maisha ya kina mama hawa kwani kila jambo linawezekana nakupongeza (Mrisho) Gambo kwa kuwawezesha wanawake hawa,” alisema.

Gambo ambaye ni mkuu wa Mkoa wa Arusha alisema mkopo huo unatolewa bila kujali itikadi ya vyama na wanaokopeshwa wamepatikana kutokana na utaratibu uliofanywa katika ofisi za mitaa na kata 25 za jiji la Arusha.

Kuhusu kina mama hao waliokopeshwa, mkuu wa Wilaya ya Arusha, Gabriel Daqqaro aliwaelezea kuwa ni kama hewa ya oksijeni kwani wanahakikisha mahitaji yote ya familia yanapatikana ikiwamo kubuni biashara za kujikwamua kiuchumi.