Washindi wa uandishi wa mashairi kujulikana wiki ijayo

Muktasari:

  • Lengo la shindano ni kukuza Kiswahili na uandishi wa mashairi

Dar es Salaam. Washindi wa tuzo ya ushairi ya Ebrahim Hussein watatangazwa Septemba 23 katika hafla ya kuwazawadia itakayofanyika katika ukumbi wa Makumbusho ya Taifa, jijini Dar es Salaam.

Taarifa iliyotolewa na waandaaji imeeleza kuwa hii ni mara ya tatu kwa tuzo hiyo kutolewa. Taarifa hiyo inabainisha kwua tuzo hiyo ilibuniwa kama njia ya kuendeleza na kukuza ushairi na lugha ya Kiswahili.

Tuzo hiyo imeanzishwa kutokana na matakwa ya mtengeneza filamu raia wa Canada, marehemu Gerald Belkin, ambaye pia alitaka iitwe kwa jina la rafiki yake, mshairi maarufu na muandaaji wa filamu, Profesa Ebrahim Hussein.

Kamati ya Usimamizi ya Tunzo ya Ushairi ya Ebrahim Hussein, ikiongozwa na Mwenyekiti wake Demere Kitunga, imeendesha shindano hili kwa kushurikiana na Tanzania Gatsby Trust (TGT) na Mkuki na Nyota Publishers.

Shindano hili la tatu lilianza rasmi Novemba 4, mwaka jana na kukamilika April 30, ambapo jopo la majaji, likiongozwa na Profesa Mugyabuso Mlinzi Mulokozi wa UDSM, lilipitia kazi zote zilizowasilishwa.