Wasomi wanena uchaguzi wa mameya Dar

Muktasari:

Katika utaratibu wa sasa, mameya na wenyeviti wa halmashauri huchaguliwa na madiwani, madiwani wa viti maalumu, wabunge wa majimbo wa kuchaguliwa, wabunge wa viti maalumu na wabunge wa kuteuliwa.

Dar es Salaam. Baada ya kuibuka malumbano katika  uchaguzi wa meya Manispaa za Kinondoni na Ubungo baina ya CCM na vyama vinavyounda Ukawa, wasomi wameshauri kanuni zibadilike ili wanaochagua meya wawe madiwani wa kuchaguliwa pekee.

Katika utaratibu wa sasa, mameya na wenyeviti wa halmashauri huchaguliwa na madiwani, madiwani wa viti maalumu, wabunge wa majimbo wa kuchaguliwa, wabunge wa viti maalumu na wabunge wa kuteuliwa.

Juzi, madiwani wa Chadema na CUF katika Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni walisusia uchaguzi wa meya kupinga wabunge walioteuliwa na Rais John Magufuli kushiriki kupiga kura, kwa kuwa walihamishwa kutoka Manispaa za Ilala na Ubungo kuiwezesha CCM ishinde umeya wa Kinondoni.

Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM),  Dk Benson Bana amesema utaratibu unaotumika sasa ndiyo unachelewesha maendeleo ya wananchi kwa sababu viongozi wanatumia muda mwingi kulumbana ili vyama vyao vishinde.

 Profesa wa Chuo Kikuu Huria (OUT), Reuben Niville amesema wananchi wanacheleweshewa maendeleo kwa sababu ya malumbano ya kila chama kutaka kuongoza halmashauri.