Wataalamu: Kupenda ngono kupita kiasi ni ugonjwa wa akili

Muktasari:

  • Wameeleza kwa nini mtu anapenda ngono sana na madhara yake

Wataalamu wa magonjwa ya mfumo wa uzazi wameeleza kuwa tabia ya kupenda ngono kupitia kiasi ni ugonjwa wa akili ujulikanao kwa jina la ‘mania’ (sexual disorder).

Akizungumza na Mwananchi, daktari bingwa wa magonjwa ya kinamama na uzazi kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Colman Living amesema kufanya ngono mara kwa mara huimarisha ubongo lakini kupita kiasi husababisha madhara mbalimbali kwa mwili.

“Kiafya kuna madhara ikiwemo maambukizi ya magonjwa kama yapo sambamba na kukinai tendo, lakini hapohapo kuna mwingine anakuwa na  hulka ya kupenda tendo hilo kwa sababu ni mgonjwa tunaita ‘sexual disorder’ au kitaalamu unaitwa ‘mania’ huu ni ugonjwa wa akili kwamba yeye anakuwa hatosheki hivyo anafanya mara kwa mara na wakati mwingine na watu tofauti,” alisema Dk Colman.

Akielezea madhara kwa wanawake, Dk Colman alisema kwa anayependa tendo hilo licha ya kuchanika sehemu za siri, inategemea anafanya na watu wangapi, kama ni tofauti anaweza kupata magonjwa mbalimbali.

Alisema kufanya tendo la ngono sana humfanya mwanamke kuwa katika hatari kubwa ya kupata mimba zisizotarajiwa ambazo wakati mwingine zinaweza kuambatana na kifafa cha mimba, kuathirika kiuchumi sababu mama atakuwa na watoto wengi ambao hawezi kuwapa mahitaji ya muhimu ikiwemo elimu, chakula na matibabu.

“Kwa wanawake saratani za njia ya uke huwaathiri zaidi hasa ile ya shingo ya kizazi ambayo kwa ujumla wake karibu asilimia 90 ya aina hizi za saratani husababishwa na virusi vya HPV ambavyo huambukizwa au kuenezwa kwa njia ya ngono kama ambavyo anapata maradhi mengine kama Hepatitis B, HIV na mengine yasababishwayo na ngono zembe,” alisema Dk Colman.

Hata hivyo alifafanua kuwa ngono kupita kiasi husababisha maambukizi mengi katika njia mbalimbali za mwili zilizowazi kama mdomoni, kwenye uke na sehemu ya haja kubwa.

Akizungumzia hilo Mkurugenzi wa Manundu Dispensary iliyopo Korogwe, Dk Ally Nzige amesema ikiwa mwanaume atafanya ngono mara kwa mara inamweka katika nafasi kubwa ya kuepukana na magonjwa mbalimbali yasiyoambukiza, lakini asipitilize kiwango na kubadilisha wapenzi.

Alisema kwa kawaida mtu anatakiwa kufanya tendo la ngono angalau mara tatu kwa wiki ni kiwango kizuri kwa afya.

“Umri sahihi kwa mwanaume kuanza kuwa tayari kwa tendo ni miaka 18 mpaka 35, hapa tunategemea kwamba awe ameshafanikiwa hata kupata watoto vinginevyo na hapo huyo atakuwa na matatizo ikiwa hatataka kujihusisha na tendo hilo hasa baada ya miaka 22,” amesema.

Dk Nzige amesema mwanaume anapokwenda zaidi ni kitu ambacho hakina shida ila inategemea na huyo patna amekubali au anamkomoa.

“Lakini hii inamtaka mtu mwenye afya iliyokuwa nzuri, pamoja na hayo inasaidia mtu kutulia kwa wale ambao wapo kwenye ndoa pia hawa wanachelewa kupata matatizo mengi, lakini watu ambao hawajaoa wala kuolewa wanapata magonjwa mbalimbali ya msongo wa mawazo, lakini ni suala la msingi kuwa na utulivu katika ndoa kwani kama huna ratiba nzuri ya maisha vitu vingine vitakushinda,” amesema Dk Nzige.

Hata hivyo amesema hakuna madhara kwa mwanaume kufanya tendo la ndoa kupita kiasi, lakini iwapo atafanya na watu tofauti anaweza kupata maradhi mbalimbali yanayoambukizwa kwa njia ya ngono.