Wataalamu wanakosea kusoma bili za maji za wateja

Muktasari:

Kero hii iliyopo maeneo mengi nchini huenda ikapata suluhu siku za karibuni baada ya wakurugenzi wa mamlaka za maji kufahamishwa juu ya hilo na kutakiwa kuchukua hatua.

Dodoma. Kilio cha wananchi wanaozidishiwa bili za maji kwa mwezi tofauti na matumizi halisi, imebainika kinatokana na makosa ya wataalamu wa kusoma mita na kuingiza taarifa kwenye mfumo wa kompyuta.

Kero hii iliyopo maeneo mengi nchini huenda ikapata suluhu siku za karibuni baada ya wakurugenzi wa mamlaka za maji kufahamishwa juu ya hilo na kutakiwa kuchukua hatua.

Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mhandisi Isaac Kamwere alipokuwa anajibu swali la Mbunge wa Songea Mjini, Leonidas Gama aliyewasilisha kero ya wananchi wake kubambikiwa gharama kubwa zisizoendana na uhalisia.

Akieleza taarifa zilizopo wizarani, Waziri huyo alisema makosa mawili yamegundulika na yanafanyiwa kazi haraka iwezekanavyo.

"Kuna service charge, wataalamu hawa walikuwa wanatoza gharama za kuwa na mita hata kama mteja hajapata maji. Hii tumeona si sawa. Waziri amewaita wakurugenzi wote na kuwaagiza kurekebisha suala hili," amesema.

Amefafanua pia kuhusu usomaji wa mita kwamba: "Walikuwa (wanaingiza) wana-punch kwenye kompyuta zaidi ya maramoja hivyo kuzidisha gharama hizo mara mbili."