Watanzania, Wanigeria wanaswa na dawa za kulevya

Kaimu Kamishna wa Usimamizi na Udhibiti wa Idara ya Uhamiaji, Kagimbo Hoseah akionyesha paspoti za watuhumiwa.

Muktasari:

Uhamiaji yasema uchunguzi ukikamilika watafikishwa mahakamani.

Dar es Salaam. Watanzania watatu na raia watano wa Nigeria wanashikiliwa na Idara ya Uhamiaji wakidaiwa kupatikana na dawa za kulevya zikiwamo Heroin, Cocaine, bangi na mashine ya kutengeneza dawa hizo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Februari 17,2018 usiku makao makuu ya Uhamiaji, Kaimu Kamishna wa Usimamizi na Udhibiti wa Mipaka, Kagimbo Hoseah amesema watuhumiwa wamekamatiwa eneo la Masaki jijini Dar es Salaam.

Hoseah amewataja Watanzania kuwa ni Ruth Kabezi, Lucy Adolf na Lizzy Minja ambaye ni wakili wa kampuni ya Law Associates.

Raia wa Nigeria wametajwa kuwa ni, Bisola Adeyemi, Olasunkanmi Kayode, Aaron Ejeh, Obina Nwauba na Darlington Nwauba ambaye ni mhitimu wa Shahada ya Sayansi ya Kompyuta (Computer science) kutoka Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Kampala tawi la Tanzania.

“Tunaendelea na uchunguzi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi, tutakapokamilisha hatua zaidi za kisheria zitachukuliwa ikiwamo kuwafikisha mahakamani,” amesema Hoseah.