Watoto wa familia moja wachinjwa, miili yakutwa kichakani

mkuu wa Wilaya Bukoba Mkoa wa Kagera,  Deodatus Kinawilo 

Muktasari:

Watoto wawili wa familia moja wamechinjwa na miili yao kutupwa kichakani katika kijiji cha Mashule wilayani Bukoba Mkoa wa Kagera, ikiwa ni baada ya kupotea kwa siku moja


Bukoba. Watoto wawili wa familia moja wamechinjwa na miili yao kutupwa kichakani katika kijiji cha Mashule wilayani Bukoba Mkoa wa Kagera, ikiwa ni baada ya kupotea kwa siku moja.

Akizungumza na MCL Digital leo Oktoba 23, 2018 mkuu wa Wilaya hiyo,  Deodatus Kinawilo amethibitisha tukio hilo na kubainisha kuwa amewaagiza polisi kufanya uchunguzi na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.

Amewataja watoto hao kuwa ni Auson Respikius (7) na Alistidia Respikius (5) walioondoka nyumbani Jumapili Oktoba 21 na miili yao kupatikana jana.

Baba wa watoto hao,  Respikius John amesema waliaga wanakwenda kucheza na wenzao, aliwaogesha na kuwaandalia nguo.

Amesema baada ya kucheza walirejea nyumbani jioni na kubadili nguo na kuondoka tena lakini hawakuonekana hadi miili yao ilipokutwa kichakani.