Watu sita tu wana mamlaka kutoa adhabu

Muktasari:

Tume ya Utumishi wa Umma imetaja mamlaka sita zenye dhamana na madaraka ya kuwachukulia hatua za kinidhamu watumishi wa umma kisheria ikiwa pamoja na kufuta nafasi za madaraka.

Dar es salaam. Tume ya Utumishi wa Umma imetaja mamlaka sita zenye dhamana na madaraka ya kuwachukulia hatua za kinidhamu watumishi wa umma kisheria ikiwa pamoja na kufuta nafasi za madaraka.

Vilevile, Tume hiyo imezitaka mamlaka za nidhamu zote kuzingatia sheria, kanuni pamoja na taratibu wakati wa kutekeleza majukumu yao kwani kwa kufanya hivyo, watumishi wanaotuhumiwa kufanya kosa watatendewa haki.

Tume ya Utumishi wa Umma imetoa maelekezo hayo siku chache baada ya viongozi wengi katika Serikali ya Awamu ya Tano wakiwamo wakuu wa mikoa na wilaya kuwachukulia kiholela hatua za nidhamu watumishi wa umma wakati baadhi hawana mamlaka hayo kisheria.

Baadhi ya wakuu wa mikoa wamekuwa wakiwasimamisha watumishi hadharani tena kwa kusikiliza malalamiko ya upande mmoja bila kuwapa walalamikiwa nafasi ya kujitetea, na wakati mwingine kudhalilishwa katika mikutano.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Katibu Msaidizi Tume hiyo, Enos Mtuso alisema kwa kuzingatia Sheria ya Utumishi wa Umma Na 8 ya mwaka 2002 na kanuni zake za mwaka 2003 madaraka ya kuwachukulia hatua za kinidhamu watumishi wa umma yako chini ya watu wachache.

“Sheria ya Utumishi wa Umma Na 8 ya mwaka 2002 ilitungwa ili kuweka misingi ya kisheria katika kutekeleza malengo ya Sera ya Menejimenti na Ajira katika Utumishi wa Umma iliyopitishwa na Serikali mwaka 1998. Sheria hii ndiyo inayotoa uwezo kwa mamlaka za kinidhamu mbalimbali katika utumishi wa umma na kuweka misingi ya namna masuala hayo yanavyopaswa kushughuliwa,” alisema.

Mtuso alizitaja mamlaka hizo kuwa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Tamisemi), Katibu Mkuu Kiongozi, watendaji wakuu, wakuu wa idara na divisheni, na mamlaka za Serikali za Mitaa (Baraza la Madiwani).

Lakini alipoulizwa mkuu wa mkoa anapata wapi mamlaka ya kuwafukuza kazi watumishi wa umma na kuwadhalilisha mbele ya hadhara, Mtuso alisema wao kama Tume hawana mamlaka ya kuzungumzia jambo hilo kwani kwa kufanya hivyo watakuwa wanakiuka maadili na kwamba suala hilo liko chini ya Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

Kauli ya Tume iliwekewa uzito na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Tamisemi), Seleman Jaffo ambaye amewataka wakuu wa idara kuacha kuwanyanyasa wafanyakazi kwani hali hiyo inasababisha wafanye kazi kwa hofu ya kutumbuliwa.

Akizungumza baada ya kuwatembelea watumishi wa umma wa Manispaa ya Ilala, jijini Dar es Salaam jana, Jaffo alisema wizara yake itatoa ushirikiano kwa watumishi wote wanaofanya kazi kwa bidii.

Katika hatua nyingine, Mtuso alitoa takwimu za mashauri ya nidhamu yaliyochukuliwa hatua katika kipindi cha 2014/2015 na 2015/2016 akisema jumla ya watumishi wa umma 249 sawa na asilimia 75 ya mashauri yote yaliyowafikia wakiwamo walimu 209 walifukuzwa kazi kwa makosa yaliyothibitika.

Alisema Watumishi hao wamefukuzwa kazi kwa makosa mbalimbali ikiwamo, kukiuka maadili ya kazi, kutotekeleza majukumu, ubadhilifu, rushwa, wizi wa fedha na mali, udanganyifu, matumizi mabaya ya madaraka, uzembe, utovu wa nidhamu huku utoro kazini ukiwa na idadi kubwa ya waliofukuzwa kazi.

“Utoro kazini ni changamoto kubwa inayotukabili na ndiyo mashauri yake mengi yanathibitika, unakuta mtumishi haendi kazini siku tano na kuendelea bila sababu maalumu wala hatoi taarifa yoyote kwa waajiri wake kuwa anashida gani,” alieleza.