Watumishi EAC watinga mahakamani

Katibu mkuu wa jumuiya ya Afrika Mashariki Balozi Liberat Mfumukeko.

Muktasari:

  • Kesi hiyo wameifungua katika Mahakama ya Haki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ) kitengo cha awali.

Arusha. Wafanyakazi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), wamefungua kesi kumshtaki Katibu Mkuu wa jumuiya hiyo kwa madai ya kuvunja mikataba ya ajira.

Kesi hiyo wameifungua katika Mahakama ya Haki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACJ) kitengo cha awali.

Wafanyakazi watatu kutoka Idara ya Amani na Usalama wanadai Juni 17, Katibu Mkuu huyo alivunja mikataba yao ya ajira kinyume na agizo la Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki waliyoyatoa kwenye mkutano wa nyongeza wa 31 na kwa kuzingatia Kanuni  ya 96 ya taratibu za wafanyakazi wa EAC ya mwaka 2006.

Wanadai kuwa walipokea barua kutoka Masjala ya EAC yenye notisi ya miezi mitatu ya kusitishwa kwa ajira zao iliyowekwa saini na katibu mkuu huyo, huku ikieleza kuwa EAC haina fedha za kuendeleza mradi wa APSA unaopata fungu kutoka Umoja wa Ulaya (EU)  kupitia Umoja wa Afrika (AU).