Watumishi Wizara ya Elimu kortini kwa uhujumu uchumi

Muktasari:

  • Miongoni mwa mashtaka hayo ni uhujumu uchumi, ubadhirifu, ufujaji  na kusababisha hasara ya mamilioni.
  • Akiwasomea hati ya mashtaka yanayowakabili  jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbroad Mashauri, Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Emmanuel Jacobo amewataja washtakiwa hao kuwa ni Mkurugenzi wa Elimu, Baraka Issa,  Mhasibu, Emmanuel Mayuma, Naibu Mkurugenzi wa Elimu, Hellen Lihawa  na Mhasibu Msaidizi, Mbarouk Dachi.

Dar es Salaam. Watumishi wanne wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi  ambayo sasa inaitwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia,  wamefikishwa Mahakama  ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka saba.

Miongoni mwa mashtaka hayo ni uhujumu uchumi, ubadhirifu, ufujaji  na kusababisha hasara ya mamilioni.

Akiwasomea hati ya mashtaka yanayowakabili  jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbroad Mashauri, Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Emmanuel Jacobo amewataja washtakiwa hao kuwa ni Mkurugenzi wa Elimu, Baraka Issa,  Mhasibu, Emmanuel Mayuma, Naibu Mkurugenzi wa Elimu, Hellen Lihawa  na Mhasibu Msaidizi, Mbarouk Dachi.

Jacobo amedai kuwa Julai 16, 2014  katika ofisi za Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ambayo kwa sasa ni Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, washtakiwa hao wakiwa waajiriwa wa wizara hiyo walitumia nyaraka za uongo kwa lengo la kumdanganya mwajiri wao.