Wawili wafa maji wakiwa katika ibada

Muktasari:

  •  Miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali ya Huruma kwa uchunguzi zaidi

     

Rombo. Watu wawili wamefariki dunia kwa  kuzama katika mto Ungwasi wakati wakiwa kwenye ibada ya ubatizo.

Kutokana na tukio hilo, Jeshi la Polisi mkoani Kilimanjaro, linawashikilia watu watatu akiwamo mchungaji wa Kanisa la Siloamu wilayani Rombo kwa uchunguzi kwa madai kuwa waumini hao walizama wakati wakiwa katika ibada iliyoandaliwa na kanisa hilo.

Kamanda wa Polisi mkoani humo, Hamis Issah amesema tukio hilo lilitokea juzi saa saba mchana, kwenye mto Ungwasi uliopo Kijiji cha Keni Kata ya Manda chini wilayani hapa.

Issah amewataja waliofariki dunia kuwa ni Gasper Utoh (47) na Proches Mrema (30).

Kamanda amesema miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali ya Huruma kwa uchunguzi zaidi.

Akielezea tukio hilo, Mkuu wa wilaya hiyo Agness Hokororo amesema waumini hao walifariki dunia wakati wakibatizwa.