Waziri Mkuu aagiza wakala wa majengo Mara kukamatwa

Muktasari:

  • Amesema mhandisi huyo anakamatwa kutokana na kushindwa kutekeleza ujenzi wa mradi wa ofisi za halmashauri ya wilaya ya Butiama

 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ameiagiza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa  (Takukuru) mkoa wa Mara kumkamata na kumuhoji meneja wa wakala wa Majengo  Tanzania (TBA) wa mkoa wa Mara, mhandisi Peter Salim.

Amesema mhandisi huyo anakamatwa kutokana na kushindwa kutekeleza ujenzi wa mradi wa ofisi za halmashauri ya wilaya ya Butiama.

Taarifa iliyotolewa leo Januari 21, 2018 na Ofisi ya Waziri Mkuu inaeleza kuwa Serikali ilitoa Sh600 milioni,  Aprili, 2017 kwa ajili ya kuanza kwa ujenzi wa ofisi za halmashauri ya wilaya hiyo, lakini hadi sasa wakala huo hajafanya kazi yoyote.

Imesema kwa maelezo yake, mhandisi Salim amesema ujenzi wa ofisi hiyo hadi kukamilika utagharimu Sh3bilioni,  kati ya Sh600milioni  zilizotolewa na Serikali Sh400milioni zimetumika kujengea msingi, kauli iliyopingwa na mkuu wa wilaya hiyo, Anna-Rose Nyamubi.

 

“Waziri mkuu siyo kweli kwamba kuna kazi inayoendelea bali kilichopo pale ni mashimo ambayo hayajulikani ni ya nini. Pia kuna jengo moja lilijengwa kwa mabati kama stoo na hakuna mafundi wanaoendelea na kazi,” amesema Nyamubi.

 

Pia, Waziri Majaliwa amemuagiza kaimu katibu tawala wa mkoa wa Mara,  Raphael Nyanda kutuma timu ya wakaguzi kwenda kufanya ukaguzi maalumu katika ofisi ya mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Butiama.

 

Amesema halmashauri hiyo imekuwa na tabia ya kutumia fedha za miradi mbalimbali ya maendeleo zinazotolewa na Serikali katika shughuli nyingine jambo ambalo ni kinyume cha sheria.

 

Waziri Mkuu ametoa agizo hilo jana Januari 20, 2018 wakati akizungumza na watumishi na madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Bitiama.

 

Pia, aliagiza kuchunguzwa kwa mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Butiama, Solomon Ngiliule pamoja na mweka hazina wa halmashauri hiyo, Masanja Sabuni na ofisa manunuzi, Robert Makendo.

 

Amesema viongozi hao wanatakiwa wachunguzwe kutokana na matumizi yasiyoeleweka ya fedha za miradi ya maendeleo zinazotolewa na Serikali zikiwemo Sh12milioni walizotumia kuandaa taarifa ya halmashauri hiyo.

 

Amesema fedha nyingine ni Sh70milioni za elimu maalumu, Sh288milioni  za mradi wa maji Butiama ambazo zote hazijulikani zimetumikaje.

 

“Hatuwezi kuvumilia vitendo hivi fanyeni uchunguzi na naomba taarifa yake mara mtakapokamilisha,” amesema.