Waziri awaonya ma-RC, DC uwekaji kiholela mahabusu watumishi

Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu

Muktasari:

  • Kisha, Septemba 16 alifuata Naibu waziri wa wizara hiyo, Selemani Jafo aliyewataka wakuu wa mikoa na wilaya kuitumia vizuri sheria inayowapa mamlaka ya kuwaweka ndani watu katika maeneo yao.

Bagamoyo. Alianza aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Tamisemi), George Simbachawene kuwataka wakuu wa mikoa na wilaya kutekeleza majukumu yao huku wakijiweka kando na uwekaji mahabusu watu mara kwa mara.

Kisha, Septemba 16 alifuata Naibu waziri wa wizara hiyo, Selemani Jafo aliyewataka wakuu wa mikoa na wilaya kuitumia vizuri sheria inayowapa mamlaka ya kuwaweka ndani watu katika maeneo yao.

Jana, Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu aliwataka wakuu hao kuacha tabia ya kuwaweka mahabusu watumishi wa umma kwa makosa ya kitaaluma.

Ummy alitoa wito huo mjini hapa wakati akizindua majengo la wodi ya wazazi na matibabu ya dharura katika Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo yaliyojengwa kwa udhamini wa Taasisi ya Dhi Nureyn.

Alisema makosa kama hayo yanapaswa kushughulikiwa na mamlaka wanazofanya kazi chini yake, lakini kitendo cha kuwaweka ndani kinawaondolea morali na ali ya kufanya kazi. “Nakushukuru mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo sijawahi kusikia umefanya kitendo cha namna hiyo. Ukiona makosa ya kitaaluma walete juu tutawashughulikia,” alisema Ummy.