Wema Sepetu, TID na wenzao waendelea kushikiliwa polisi

Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro akizungumza na waandishi wa habari  jana kuhusiana na wasanii waliofika katika kituo kikuu cha polisi kwa ajili ya mahojiano. Picha na Omar Fungo

Dar es Salam.Wakati macho na masikio ya Watanzania wakisubiri kusikia hatma ya wasanii wanaodaiwa kujihusisha na dawa za kulevya, wasanii wanne waliofika Kituo Kikuu cha Polisi bado wanashikiliwa na jeshi hilo kwa mahojiano zaidi.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro amesema kuwa bado wasanii hao Wema Sepetu, Dogo Hamidu, Khalid Mohamed (TID), na mtangazaji maarufu wa Clouds TV Babuu wa Kitaa bado wanashikiliwa na jeshi  hilo.

“Bado tunawashikilia kwa mahojiano zaidi,” amesema Sirro kwa kifupi.

Wasanii wengine waliotajwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda ambao wanatakiwa kufika kituoni Jumatatu ni Vanessa Mdee, Tunda na watu wengine Halidali Kavila, Amani, Kashozi na Omry Sanga.