Zitto adai ahadi ya kuleta bombadier mpya yayeyuka

Muktasari:

  • Mwaka jana, Serikali ilinunua ndege mbili aina ya bombadier na kuzikabidhi kwa Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) kwa ajili ya uendeshaji.

Dar es Salaam. Ahadi ya Serikali ya kununua ndege ya tatu ambayo ilitakiwa kufika nchini Julai, imeshindwa kutekelezwa hadi sasa na Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe amehoji kulikoni.

Mwaka jana, Serikali ilinunua ndege mbili aina ya bombadier na kuzikabidhi kwa Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) kwa ajili ya uendeshaji.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa na Naibu wake, Mhandisi Edwin Ngonyani kwa nyakati tofauti walikaririwa wakisema ndege hiyo itawasili Julai na kufanya idadi ya ndege za ATCL kuwa nne.

Hata hivyo, Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe katika ukurasa wake wa Twitter jana alimuliza Profesa Mbarawa kuhusu ndege hiyo.

“Serikali iliahidi bungeni kuwa Julai 2017 mtapokea ndege nyingine ya Bombadier, leo ni Agosti iko wapi, lini itafika, nini kimetokea,” aliuliza Zitto

Profesa Mbarawa alimjibu kuwa “ni kweli kabisa ahadi ilikuwa Julai kuna taratibu za mwisho zinafanywa kabla ya kuwasili hivyo itawasili tu.”

Baada ya majibu hayo, Zitto alitaka kufahamu kutoka kwa Profesa Mbarawa ni lini ndege hiyo itawasili.

“Sababu za kuchelewa ni nini, delay (kuchelewa) ya mwezi mzima siyo dalili nzuri ndugu waziri, ni kwa sababu hamjalipa au zimezuiwa na wanaotudai,” aliuliza Zitto.

Alipopigiwa simu ili azungumzia suala hilo, Profesa Mbarawa hakupatikana lakini Naibu wake, Mhandisi Ngonyani alitaka aachwe ili atafute taarifa halisi za ndege hiyo.