Zitto asakwa

Muktasari:

Katibu wa Bunge amesema anatakiwa afikishwe mbele ya kamati.

 

 Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT –Wazalendo), Zitto Kabwe anatafutwa ili akamatwe na kufikishwa mbele ya Kamati ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge.

Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah amesema leo Jumatano kuwa, Zitto alipewa barua ya wito wa kufika mbele ya kamati hiyo baada ya Spika Job Ndugai kuagiza hilo lifanyike lakini hadi sasa hajaitikia wito huo.

Amesema kamati bado ipo mjini hapa ikiendelea na shughuli baada ya vikao vya Bunge kuahirishwa na inamsubiri.

Dk Kashililah amesema Zitto alipewa barua ya wito lakini alikuwa na udhuru kwa kuwa siku aliyotakiwa kufika mbele ya kamati alikuwa na kikao cha halmashauri

lakini kesho yake angefika kuitika wito.

“Wakati wanamsubiri mara wakamsikia yuko Nairobi (Kenya), kamati inaendelea kumsubiri. Kamati inasema imeagiza wawaone wasije kusema wanatoa hukumu

na wao hawapo,” amesema.

Zitto amepelekwa na Spika Ndugai mbele ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge inayoongozwa na Mbunge wa Newala Mjini (CCM), George Mkuchika akidaiwa kutamka kwenye mitandao ya kijamii kuwa Bunge limewekwa mfukoni na mhimili fulani.

Maneno hayo anadaiwa kuyasema wakati  kamati mbili za Spika kutathmini mfumo wa uchimbaji, usimamizi, umiliki na udhibiti wa madini ya Tanzanite na almasi zilipowasilisha taarifa.