Zitto ataka mkutano wa kimataifa wa maridhiano

Muktasari:

Asema katika mkutano huo zitajadiliwa changamoto zote za kisiasa zinazoikabili nchi kwa sasa.

 


Arusha. Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe ametaka uitishwe mkutano wa kitaifa wa maridhiano ili kujadili hali ya kisiasa na usalama nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumamosi, Februari 24, 2018 jijini Arusha, Zitto amesema katika mkutano huo zijadiliwe changamoto zote za kisiasa na kukubaliana kanuni za demokrasia ya vyama vingi. 

"Hii ni kutokana na dhahiri kuwa mfumo wa vyama vingi nchini upo hatarini zaidi kuliko wakati wowote,” amesema.

Amesema mkutano huo unatakiwa kuwashirikisha pia viongozi wa vyama vya wafanyakazi, wafanyabiashara, wakulima na wafugaji.

Amebainisha kuwa hali ya kisiasa sasa si ya kuwaachia wanasiasa pekee kwa kuwa pia inahusu uhai wa watu na wengine ambao hata hawajihusishi na siasa.

Zitto yupo mkoani hapa kutembelea kata ambazo zina madiwani wa chama hicho na kuzungumza na wajumbe wa kamati za maendeleo za kata hizo.