VIDEO-Zitto awashukia mawaziri

Muktasari:

  • Amesema kinachofanywa na mawaziri ni kinyume cha sheria, nayo imeweka adhabu kwa makosa hayo 

Dodoma.Mbunge wa Kigoma (ACT-Wazalendo), Zitto Kabwe amesema kitendo cha mawaziri kujibu hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), ni kinyume cha Sheria ya Ukaguzi wa Hesabu za Umma na kifungu 38 (1 na 2).

Akizungumza leo Aprili 15 mjini hapa, Zitto amesema kifungu hicho kinaeleza namna hoja hizo zinavyotakiwa kujibiwa na kwamba mawaziri wamekuwa hawatajwi kabisa katika kifungu hicho.

“Wanaopaswa kujibu hoja za CAG ni maofisa masuhuli ambao ni makatibu wakuu wa wizara, siyo kujibu kwa kuita mikutano na wanahabari bali kujibu kwa kutokea katika kamati (za Bunge za Hesabu),” amesema.

Amesema kinachofanwa na mawaziri ni kinyume cha sheria na kwamba, sheria imeweka adhabu kwa makosa hayo  ya juu  kabisa ikiwa ni kifungo cha miaka miwili jela au faini ya Sh5 milioni.

“Nawasihi mwenyekiti wa kamati ya PAC na mwenyekiti wa kamati ya LAAC wafikishe jambo hili kwa Spika ili  amuandikie Waziri Mkuu kumweleza kuwa, mawaziri wanavunja sheria. Kinachonisikitisha ni kuwa baadhi ya mawaziri waandamizi ndiyo wanaongoza zoezi hili,” amesema.

Amesema anafahamu wanachokifanya mawaziri hao ni kuhamisha mjadala, kwa kuwaondoa watu katika hoja za msingi ambazo CAG ameziibua ili zisijadiliwe.