Zitto awataka wabunge wasikubali kupiga porojo

Muktasari:

Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT Wazalendo) Zitto Kabwe amewatahadharisha wabunge kuwa kitu kimoja na kushirikiana katika kuisimamia ipasavyo Serikali ili itekeleze kile wanachokubaliana

Dodoma. Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT Wazalendo) Zitto Kabwe amesema kama wabunge hawatahitaji uwajibikaji upande wa Serikali watakuwa wanapiga porojo kutokana na kutotekelezwa kwa mambo wanayokubaliana.

Akichangia Mapendekezo ya Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa mwaka wa fedha 2019/20, leo Alhamisi Novemba 8, 2018, Zitto amesema katika mpango wa mwaka 2016 walijadiliana na kukubaliana Serikali ikatenge Sh13.2 trilioni kwa ajili ya mpango huo lakini walitoa Sh5 triloni.

Amesema mwaka 2017 walikubaliana zitengwe Sh12 trilioni lakini zilizotolewa zilikuwa ni Sh 6trilioni tu.

“Hii inaonyesha kama hatutakuwa makini na kuhitaji uwajibikaji upande wa Serikali tutakuwa tunapiga porojo. Kwa sababu kile tulichokubaliana kikafanywe wenzetu ambao tumekubaliana nao hawafanyi,” amesema.  

Amesema Serikali ina tatizo kwenye taarifa za uhasibu na kwamba ukitazama taarifa zilizopo sasa inaonyesha kuwa wanarudi katika tatizo kama la upotevu wa Sh1.5 trilioni.

Amesema ukiangalia katika taarifa ambazo zimetolewa na Serikali za makusanyo hadi Juni, 2018 na taarifa ya fedha ambazo Serikali imezitoa kwenda kwenye mafungu kuna tofauti ya Sh2.1trilioni.