Uwekezaji wa TCC wawakuna wabunge

Muktasari:

  • Pongezi hizo zilitolewa wakati wa ziara ya kamati hiyo iliyoratibiwa na Shirikisho la Viwanda Tanzania (CTI), ikishirikisha naibu waziri wa wizara hiyo, Stella Manyanya na watendaji wengine.

Dar es Salaam. Kamati ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira imeipongeza kampuni ya Sigara Tanzania (TCC Plc) kwa utekelezaji wa malengo ya ubinafsishaji na kuendeleza azma ya serikali ya viwanda.

Pongezi hizo zilitolewa wakati wa ziara ya kamati hiyo iliyoratibiwa na Shirikisho la Viwanda Tanzania (CTI), ikishirikisha naibu waziri wa wizara hiyo, Stella Manyanya na watendaji wengine.

Mwenyekiti wa kamati hiyo, Suleiman Sadiq aliipongeza TCC Plc kwa mafanikio makubwa na kwamba, wameridhishwa na walichokiona na kuutaka uongozi na wafanyakazi kuendeleza kazi hiyo nzuri.

“TCC Plc ni mfano mzuri unaopaswa kuigwa na wengine kwani imekuwa imara katika ulipaji wa kodi serikalini... kamati imezichukua changamoto zenu tutaishauri Serikali inavyostahili,” alisema.

Naye Manyanya alisema kampuni hiyo imeonyesha mfano katika mafanikio ya ubinafsishaji kwa kuwa baadhi ya mashirika yaliyobinafsishwa wakati mmoja na TCC Plc yalishindwa kujiendesha na yamekufa.

Mtendaji mkuu wa TCC Plc, Alan Jackson alisema kwa mwaka jana walilipa serikalini Sh227 bilioni zikiwa ni kodi ya ongezeko la thamani (Vat), mapato na ushuru wa bidhaa.