Zitto azidi kupigilia msumari ushuru wa korosho

Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe akizungumza bungeni alipokuwa akichangia mjadala wa kupitisha Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2018/2019, jijini Dodoma leo. Picha na Edwin Mjwahuzi

Muktasari:

  • Ametoa kauli hiyo leo katika mjadala wa bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2018/19

Dodoma. Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), Zitto Kabwe amesema Serikali inapaswa kuwa makini na zao la korosho kwa maelezo kuwa kitendo inachotaka kufanya cha kuchukua asilimia 65 ya fedha za mauzo ya korosho nje ya nchi, ni hatari.

 

Akizungumza katika mjadala wa bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha wa 2018/19 leo Ijumaa Juni 22, 2018 bungeni mjini Dodoma, amesema  mfumo wa Bunge ni mfumo wa Kamati, kwamba kamati za chombo hicho cha Dola, zinafanya kazi kwa niaba ya wabunge wote.

 

Tayari baadhi ya wabunge wametishia kufanya maandamano iwapo Serikali haitatoa asilimia 65 ya ushuru wa mauzo ya korosho nje kwa ajili ya maendeleo ya zao hilo.

 

Pia, wabunge wamepinga mabadiliko ya Sheria ya Korosho yanayokusudiwa kufanywa na Serikali ili ushuru huo upelekwe katika Mfuko Mkuu wa Hazina.

 

Akizungumzia jambo hilo ambalo kamati ya Bunge ya Bajeti ililipinga katika maoni yake kuhusu bajeti ya Serikali mwaka 2018/19, iliyoyawasilisha bungeni Juni 18, 2018, Zitto amesema ni vyema jambo ambalo wabunge wanakuwa na mashaka nalo, likafanyiwa kazi.

 

“Leo ukija bungeni uwapinga wabunge wanaolima korosho, kesho utakuwa na jambo lako utakosa wa kukuunga mkono na busara ni kukaa kimya,” amesema Zitto na kubainisha kuwa korosho na mazao mengine kama pamba na kahawa yamesaidia kuongeza pato la kigeni kwa Taifa.