
| Amina: Nilifanyishwa ngono nikiwa na miaka 12, sasa saratani ya kizazi inanitesa | Send to a friend |
| Friday, 27 January 2012 12:28 |
|
Maji yenye harufu humwagika kwa saa 24, hali inayomfanya Amina atumie nepi maalum au ‘diapers’ ili kuzuia maji hayo yasilowanishe shuka. Si hivyo tu, bali uvimbe huo mkubwa umeziunganisha sehemu ya haja kubwa na uke hali inayompa tabu zaidi kupata haja kubwa. Uvimbe huo, ambao humfanya atembee kwa taabu, unamsababishia asiende haja ndogo kama wanawake wengine wafanyavyo, bali kwa mtindo ambao anadai, hauelezeki. Na kubwa zaidi ni maumivu, ambayo anadai, yanafanana na mdudu anayetafuna sehemu za kiuno chake- huku wakati mwingine akihisi kisu kikali kikipita chini ya tumbo lake. Amina anakesha akilia kwa maumivu, huku akitamka maneno haya kila mara: Akiwa na umri wa miaka 31 tu, mwanamke huyu anasema amepitia machungu zaidi kuliko furaha. Na hii ndiyo historia ya maisha yake; Alizaliwa mkoani Mbeya, Wilaya ya Katumba. Awali aliishi na mama yake Rose Freddy pekee. Alipofikisha umri wa miaka minne, mama yake aliamua kumpeleka kwa baba yake. Amina anasema, maisha nyumbani kwa baba yake, mzee Samweli Shabani hayakuwa mazuri sana. Anasema, alipoona hakuna dalili ya kupelekwa shule, aliamua kutoroka, wakati huo alikuwa na umri wa miaka 10. Katika kuzunguka zunguka mjini Mbeya, Amina alikutana na mwanamke mmoja, ambaye ni askari wa Usalama Barabarani(Traffic). Anasema, askari huyo aliamua kumsaidia, lakini kwa masharti ya kuwa, Amina atamsaidia kulea watoto wake wadogo. “Nilipewa kazi ya kulea watoto wa yule mama, hakunipa ujira ingawa nilikula na kuvaa,” anasimulia. Baada ya miaka miwili, traffic yule alifariki dunia, na ikambidi Amina kukimbilia kwa Joyce Mwamkinga, maarufu kama Mama Lusi. Mama Lusi alikuwa ni rafiki wa askari yule na alikuwa akiishi katika kijiji cha Isanga. Na hapo ndipo kilipo kiini cha machungu ya Amina. Mama Lusi hakuwa na mume na wala hakuwa akifanya kazi yoyote, lakini alikuwa akitoka usiku na kurejea asubuhi. Siku moja, Mama Lusi alianzisha utaratibu mpya ndani ya nyumba hiyo. Utaratibu ambao twaweza kusema ni wa kikatili, ambao pengine ndicho chanzo cha mateso anayoyapata Amina leo hii katika kitanda hospitalini Ocean Road. “Mama Lusi alituambia, ni lazima kila mmoja alale na mwanaume ili tupate pesa ya kuishi,” Amina anasema huku akilia. Mama huyo, hakufanya hivyo kwa Amina pekee, bali hata kwa watoto wake wawili wa kike, wa kuwazaa, Tuma na Lusi. “Tuma alikuwa na miaka 14 Lusi alikuwa na miaka 16, na mimi 12, nilikuwa sisikii chochote kimapenzi, wala sijui kitendo cha ngono ni kitu gani, lakini nilifanyishwa kwa nguvu,” anasema Amina. Msichana huyu mwenye mtoto mmoja anasema, katika umri huo, alifanya mapenzi na wanaume wenye umri tofauti tofauti. “ilifikia mahala ikawa ni tabia, kwa hiyo nikazoea kuishi kwa kujiuza kimwili, “ anaeleza zaidi. Mama yangu baada ya kusikia kuwa nakaa kwa mama Lusi alikuja kutoka Katumba na kunichukua, lakini nilikuwa situlii, nakaa kidogo kwa mama , kisha natoroka narudi kwa Mama Lusi. Amina anasema, anasikitika kwa kuwa, Mama Lusi pamoja na watoto wake wote, hivi sasa wamefariki kwa ugonjwa wa UKIMWI. Chanzo cha maradhi yake Daktari wa Patholojia, wa hospitali ya Taifa ya Muhimbili Innocent Mosha anasema, Ugonjwa huu huambukizwa kama magonjwa mengine ya zinaa yaani kwa njia ya kufanya ngono, na kwa asilimia kubwa husababisha saratani ya shingo ya kizazi. Amina anasema, kwa kumbukumbu zake, alianza kuugua ugonjwa wa zinaa mwaka 2000. Wakati huo, alikuwa ndiyo ametoka kujifungua. “Nilianza kuona vitu kama sugu(wart) katika sehemu zangu za siri, kadiri siku zilivyozidi kusonga ndivyo zilivyozidi kuongezeka ukubwa zikiambatana na maumivu,” anasema Amina. Juhudi za kwenda hospitali mjini Mbeya hazikufua dafu na ilipofika mwaka 2000, Oktoba 5, alipewa rufaa ya kufika Muhimbili. Hapo alifanyiwa upasuaji wa kuondoa uvimbe huo zaidi ya mara tatu. Mwezi Desemba mwaka jana alipewa kibali cha kwenda katika taasisi ya saratani ya Ocean Road. Alipofika Ocean Road ndipo madaktari walipompasulia Amina kuwa ana saratani ya shingo ya uzazi kitaalamu(cervical cancer). Saratani hiyo ndiyo iliyomsababishia uvimbe mkubwa katika sehemu zake za siri. Nazungumza na kaka yake Amina, Joseph Nyalile (31) ambaye ametoka Mbeya ili kumuuguza dada yake kipenzi, ambaye anadai wamecheza pamoja tangu wangali makinda. “Dada yangu hana mama na mimi ndiyo ndugu yake” anasema Nyalile. Nyalilie anasema, amekuwa akilala nje ya hospitali ya Ocean Road kwa mwezi mzima sasa kwa kuwa hana ndugu hapa jijini na ameishiwa fedha kabisa. “Siku nyingine nakosa hata fedha ya kula, nikikopa basi ni kwa ajili ya Amina,” anasema. “Daktari aliposoma tu majibu ya vipimo, alitingisha kichwa, nilipomuuliza kwa nini, hakunijibu,” anasema Nyalile. |



Na Florence Majani











Comments
Uamuzi wa mama yake kumpeleka kwa baba yake, ndio mwanzo wa matatizo kwa Amina. Lakini KIINI cha tatizo, kipo kwa baba na mama yake, ambao hawakuishi pamoja kumlea Amina, kwa sababu ambazo hazijatajwa kwenye kisa hiki.
Hapa tujifunze kwamba,
* 1.Kuzaa watoto nje ya ndoa inaweza kuleta athari kubwa sana kwa mtoto siku za mbeleni.
* 2.Kuvunjika kwa ndoa kunaweza kleta athari kubwa sana kwa mtoto.
* 3.Tofauti kati ya wazazi, zinapaswa kushughulikiwa mapema, ili kurekebisha mambo kwa kumfikiria mtoto.
* 4.Kuwafanyisha ngono watoto, ni jambo baya mno, mno. Bora ukafagia barabara, ukachoma mahindi, au hata ukachimba mtaro, mtoto apate mahitaji muhimu, kutia ndani ELIMU, ili hatimaye awe salama.
* 5.Maadili yakivunjwa, madhara hayaepukiki. Tukimtii Mwenyezi Mungu kama anavyotuagiza juu ya ngono, tutakuwa salama.
* 6.Viongozi wa kidini waendelee kuhudumia watu kiroho kwa bidii, ustawi wa jamii waweke mikakati ya kupeleka elimu mpaka vijijini, juu ya malezi.
* 7.Viongozi kuanzia ngazi ya mjumbe wa nyumba kumi, Serikali za mtaa, n.k. wapite nyumba kwa nyumba kujua hali halisi za familia na kuzifuatilia. Ili panapohitajika msaada wa kiafya, kisheria na kiusalama waweze kuchukua hatua mapema.
* 8.Mtu/watu wakiona watoto walioko katika mazingira fulani magumu, hatarishi au yasiyoeleweka, watoe ushirikiano, kwa kumjulisha mjumbe au ofisi ya Ustawi wa Jamii, na ikiwezekana hata polisi. Ila wahakikishiwe USALAMA WAO na USIRI.
Japo inaweza kuwa vigumu [NENO BAYA]liza kabisa tatizo, lakini si bure, jitihada zitasaidia. Na iwekwe mikakati maalumu ya kudhibiti ongezeko la watoto wa mitaani. Mungu atabariki jitihada. Litengwe fungu maalumu na Serikali au wafadhili kwa ajili hiyo. Fungu ambalo litasimamiwa na idara kadhaa ili kuhakikisha halitumiwi kwa malengo tofauti.MUNGU TUBARIKI, TUHURUMIE, TUSAMEHE, TUONGOZE NA KUTUFUNDISHA. MSAIDIE PIA AMINA AISHI KWA MATUMAINI, NA HATA KAMA MAUTI YATAMFIKA, AKUTUMAINIE WEWE< ATUBU MAKOSA ALIYOSABABISHIW A, NA AWE TAYARI KWA AJILI YA UFALME WAKO. Sisi sote pia tujiandae kiroho, maana hata kama hatutapata kama yaliyompata Amina, lakini tunaweza kufa kwa sababu yoyote, kwa kuwa tumerithi dhambi ya Adamu, mshahara wa dhambi ni kifo. Lakini tumaini la uzima wa milele, liko kwa wote wanaojinyenyeke za mbele za Mungu.