
| Umeme; ndoto ya wananchi Kagera iliyomtesa Waziri Ngeleja | Send to a friend |
| Friday, 27 January 2012 12:31 |
|
Miongoni mwa adha kubwa kwa wananchi hao ni kutembea mwendo mrefu kutafuta huduma kama za kukoboa na kusaga nafaka huku mafundi wa fani mbalimbali wakishindwa kutumia ujuzi wao kikamilifu kujiletea maendeleo kutokana na vifaa vyao kutegemea umeme. Baadhi ya wananchi vijijini Mkoani Kagera mzigo mkubwa kwao ni kumiliki vitu kama simu za kiganjani kutokana na huduma za umeme kuwa mbali au kutokuwapo kwa nishati hiyo wakati huo wakilazimika kwenda na mabadiliko katika teknolojia ya mawasiliano. Katika ziara yake mkoani humo wiki chache zilizopita, Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja katika wilaya za Bukoba, Karagwe na Ngara mkoani humo ilithibitika dhahiri kilio cha wananchi juu ya mahitaji ya umeme. Hata katika baadhi ya vijiji Ngeleja alipokea malalamiko ya kucheleweshwa kwa ahadi za kupatiwa nishati hiyo zinazorudiwa kila mara na wanasiasa wakati wa kampeni za uchaguzi. Awali, kabla ya kuanza kwa ziara katika wilaya ya Bukoba, Ngeleja alilazimika kufanya majadiliano na viongozi wa mkoa huo kuangalia jinsi ya kumaliza aibu kwa Watanzania kwenye mpaka wa Mutukula. Tangu Uhuru hawajawahi kupata umeme ilihali umeme upo mita chache upande wa pili wa mpaka wa Uganda ambapo hulazimika kuvuka kufuata huduma ambazo zingepatikana kwao kama umeme ungekuwepo. Hatima ya majadiliano hayo ilikuwa ni kutangaza neema kwa wakazi wa Mutukula wilayani Missenyi kuwa wizara itatoa zaidi ya bilioni moja zinazohitajika ili kupeleka umeme katika eneo hilo kabla ya kumalizika mwaka huu. Kilio cha umeme Karagwe Kijiji cha Rwambaizi , Kata ya Kanoni wilayani humo ni miongoni mwa vijiji vingi ambavyo wakazi wake wamesubiri utekelezaji wa ahadi ya kupelekewa huduma ya umeme kwa muda mrefu kama walivyohaidiwa na Rais Jakaya Kikwete mwaka mmoja uliopita. Akiwa katika ofisi za CCM mjini Kayanga wilayani humo, Waziri Ngeleja alipewa taarifa ya chama kuwa ucheleweshwaji wa ahadi hiyo unaleta hofu ya kisiasa na kujenga hoja kwa wapinzani juu ya ahadi hewa za umeme. Ziara ya Ngereja ilifufua matumaini ya wakazi wa Kata za Kanoni, Kituntu ikiwamo Kijiji cha Rwambaizi ambapo alimwagiza Meneja wa Tanesco wilayani humo, Oliva Mushumbusi kuomba milioni 250 zinazohitajika kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo uliosimama tangu mwaka 2004. Kama ilivyo takribani vijiji vyote vya wilaya ya Karagwe, pia kilio cha mahitaji ya umeme kilisikika kwa wananchi wa Ngara ambao mazingira yao yanaonyesha upatikanaji wa umeme unaweza kufungua njia nyingi za kujikwamu a kiuchumi. Kuthibitisha kuwa suala la umeme ni kete muhimu kwa wanasiasa, Mbunge wa Jimbo hilo, Deogratias Ntukamazina aliwakumbusha wapigakura wa kijiji cha Rulenge kuwa kama alivyoahidi umeme na sasa alikuwa ameambatana na waziri mwenye dhamana hiyo. Anasema kwa kipindi hiki tunalazimika kuishi kwa matumaini hadi wakati huo ambapo wananchi watashuhudia matunda kamili yanayotokana na mipango thabiti ya serikali kuondokana kabisa na kero ya umeme. Kwamba ni dhamira ya serikali kuondokana na utegemezi wa uzalishaji wa umeme kwa njia ya maji na badala yake kuwekeza zaidi katika umeme wa gesi,upepo na makaa ya mawe. Anabainisha kuwa dhamira ya Serikali ni kuiunganisha mikoa ya Kagera,Kigoma na mingine katika gridi ya umeme ya taifa ambapo wilaya ya Biharamulo kama zilivyo wilaya nyingine utawaku ni wakati wa kuondokana na uzalishaji wa umeme kwa kutegemea mitambo iendeshwayo kwa mafuta ya dizeli. Akizungumzia mipango ya uzalishaji wa umeme katika maporomoko ya Rusumo wilayani Ngara, Waziri Ngeleja anasema kuwa hatua za awali za mradi huo tayari zimeanza kwa kushirikiana na nchi za Rwanda na Burundi. Anasema kukamilika kwa mradi huo ifikapo mwaka 2016 utaiwezesha Tanzania kupata megawati 30 kati ya tisini zitakazokuwa zinazalishwa katika maporomoko hayo ambapo kila nchi itapata mgao sawa. |



Na Phinias Bashaya










