MwanzoContactsEmail
Home Makala Jungukuu Kiswahili kinaathiriwa na lugha zetu za asili
BOOKMARK THIS PAGE
Kiswahili kinaathiriwa na lugha zetu za asili  Send to a friend
Thursday, 02 September 2010 14:21


Na Stephen Maina

Napenda kuwashukuru sana baadhi ya wasomaji wangu walioniletea ujumbe kwa njia ya simu za kiganjani kuhusu maoni kwa makala ninazoandika.

Maoni na mapendekezo walioniletea yamezingatiwa  na yatasaidia sana katika kuboresha makala nyingine siku za mbele kwani itanibidi kuwasambazia wasomaji wengine maoni haya ili nao wafaidike.

Kwa wale wakereketwa wa Kiswahili wanaojali matumizi fasaha ya lugha ya Kiswahili, nawaomba waendelee na juhudi zao na pia kujitahidi kuwaelekeza watumiaji wabaya wa Kiswahili popote wanapokuwa kwani haya ni mapambano makubwa. Iko siku ambapo wale wanaopiga vita ukuzaji na uendelezaji wa Kiswahili sanifu watasalimu amri na watatuunga mkono.

Kwa hiyo katika jitihada za kuendeleza mapambano hayo, nitaendelea kuyachunguza magazeti ya Kiswahili na kukosoa pale ambapo panahitajika kukosolewa kama ifuatavyo:
“ Kuna wakati palitokea kizaizai baada ya mchezaji wa Wales, Billy Wright alipookoa kwa mkono mpira uliokuwa unaelekea wavuni “
Neno kizaizai limetumika kwa makosa kwani halipo katika msamiati wa Kiswahili sanifu. Mwandishi alitakiwa kutumia neno kizaazaa kwa maana ya kuwa katika hali ya fujo ambapo watu hawasikilizani. Inawezekana mwandishi alilisikia likitumika katika mazungumzo na hakujitahidi kulifuatilia kwa kuangalia katika kamusi zilizopo.
“  Kimsingi jambo la msingi ni matajiri kuacha kutumia soka kukuza majina yao na biashara zao.”

Mwandishi alikuwa na nia njema ya kueleza jinsi watajiri wanavyotumia suala la mpira kwa malengo yao binafsi. Lakini hakuwa mwangalifu katika mpangilio sahihi wa maneno katika lugha. Alitakiwa kuandika, “ Jambo la msingi ni kuwa matajiri wanatakiwa kuacha kutumia soka kwa kukuza majina yao na biashara zao.” Neno kimsingi mwanzoni mwa sentensi halina maana.

“ Unaweza kuwafananisha na wanajeshi wanaotumwa vitani  kuikomboa nchi isivamiwe na adui.”
Katika sentensi hii neno ‘kuikomboa’ limetumiwa vibaya. Alichomaanisha hapa ni kuilinda nchi isivamiwe na adui na wala siyo kuikomboa.

Maana ya kukomboa pia kigomboa ni kumfanya mtu aliyekuwa amefungwa au aliye katika unyonge, udhalimu au kutawaliwa awe huru. Mwandishi alikuwa na maana ulinzi wa nchi. Kwa hiyo isomeke, “Unaweza kuwafananisha na wanajeshi wanaotumwa vitani kuilinda nchi yao isivamiwe na adui.”

“ Tutaendelea kufanya hivyo kwani hiyo ndiyo njia pekee ya kuinua vibaji michezo hao nchini.”
Katika sentensi hii yako makosa mawili, La kwanza ni matumizi mabaya ya neno ‘vibaji’. Neno hili lilitakiwa kuwa ‘vipaji’. Mwandishi ameathiriwa na lugha yake ya asili ambapo fonimu /p/ hutumika badala ya /b/.

Yako baadhi ya makabila hawana fonimu /b/ badala yake hutumia /p/. Tunatakiwa kujirekebisha katika tatizo hili. Pili ni matumizi ya maneno ya mwisho hayaeleweki vizuri. Maneno hayo ni ‘kuinua vipaji michezo hao nchini.’ Ilitakiwa iwe ‘ kuinua vipaji vya wanamichezo hao nchini.’

“ CCM Mkoa wa Arusha kimefanya vikao kadhaa vya siri na sasa iko mbioni kuunda kamati katika kila kata kwa mantiki ya kuondoa vitendo vya rushwa wakati wa uchaguzi.”

Maana ya neno mantiki imepotoshwa na halina maana hapa. Maana ya mantiki ni mtiririko wa fikra zilizopangwa ili kujenga hoja yenye kukubalika. Haiwezekani kusema ‘kwa mantiki ya kuondoa vitendo vya rushwa.” Inatakiwa kuandika ‘kwa lengo la au kwa madhumuni ya ‘  Kwa hiyo isomeke CCM Mkoa wa Arusha kimefanya vikao kadhaa vya siri na sasa iko mbioni kuunda kamati katika kila kata kwa lengo/madhumuni ya kuondoa vitendo vya rushwa  wakati wa uchaguzi. ”

 “ Wakati wa kampeni, mgombea anakuwa na uwezo wa kujenga visima, mashule, mahospitali na kugawa pesa huku akizunguka majimboni kwa kugawa pesa na misururu ya magari ya kukodi.”
Msomaji wa kawaida akisoma sentensi hii ataiona kuwa ni sahihi. Lakini kwa jicho la kisarufi inaonekana kuwa mwandishi alitumia viambishi “ma’ bila kuwa mwangalifu. Maneno shule na hospitali yameazimwa kutoka katika lugha ya kigeni. Neno shule lina asili ya Kijerumani (Schule) na hospitali lina asili ya lugha ya Kiingereza (Hospital).

Kwa kawaida hatuongezi kiambishi ‘ma’ mbele ya maneno haya wakati wa kuandika wingi wake.


Wako waandishi ambao wanaendelea kuongeza  kiambishi “ma” katika maneno ambayo si lazima kuwa na kiambishi  awali cha ‘ma’. Angalia sentensi ifuatayo:
“ Lakini pia ni muhimu kuchukua maamuzi yenye maana.”
Ni sahihi kuandiika , “ Lakini pia ni muhimu kuchukua uamuzi wenye maana. Kwa kweli tusipokuwa makini katika uandishi wetu tutaipotosha lugha hii na itakukuwa vigumu kurekebisha makosa ya aina hii kwa vizazi vijavyo.
“  Ni wazi umakini unapaswa kufanywa katika kuhakikisha wakulima wanasaidiwa kwa uhakika.”
Si sahihi kusema kuwa umakini unapaswa kufanywa.

Haya ni mawazo kutoka katika lugha za kigeni. Sahihi ni kusema, ‘ jitihada zinapaswa kufanywa.’ Hivyo iandikwe, “ Ni wazi jitihada zinapaswa kufanywa katika kuhakikisha kuwa wakulima wanapata misaada ya uhakika.”
“Shoo hiyo ilifanyika hoteli ya Serena mjini Unguja ilisindikizwa na wabunifu wengine wawili ambao ni Faruq

Abadallah na Mango. Ambao wote kwa pamoja walikuja na mavazi mbalimbali ya ubunifu.”
Kama tutaisoma sentensi hii kwa makini tunaweza kupata makosa kama ifuatavyo. Kwanza tuelewe kuwa Unguja ni kisiwa na wala si mji.
Mji ni Zanzibar. Vilevile shoo haiwezi kusindikizwa na wabunifu. Kinachofanyika hapa ni kuwashirikisha wabunifu. Mawazo ya kusindikiza wabunifu ni dhana ya kigeni. Suala la mwisho katika sentensi hii ni matumizi ya alama ya nukta baada ya neno Mango. Neno ‘ambao’ ni kiunganishi na aslani haliwezi kuanza sentensi. Kwa hiyo isomeke kama ifuatavyo:

“ Shoo hiyo iliyofanyika katika hoteli ya Serena mjini Zanzibar iliwashirikisha wabunifu wengine wawili ambao ni Farouq Abdallah na Mango ambao wote kwa pamoja walikuja na mavazi mbalimbali ya ubunifu.”
“ Shule hiyo yenye wanafunzi 560 ina madarasa sita na walimu 13 jambo ambalo linatishia kushuka kwa taaluma.”

Ili kuiweka sentensi hii kwa usahihi wake ilibidi kuongeza maneno machache kama ifutavyo: Ingefaa kuongeza neno ‘ ni ’ na kusomeka ‘ ni jambo ambalo linatishia…’ Pia neno ‘kiwango’ liongezwe ili isomeke ‘kiwango cha taaluma’. Kwa hiyo sentensi isomeke,
“ Shule hiyo yenye wanafunzi 560 kwa madarasa  sita na walimu 13 ni jambo ambalo linatishia kushuka kwa kiwango cha taaluma.”
0716  694240, 0754  861664


Add this page to your favorite Social Bookmarking websites
Reddit! Del.icio.us! Mixx! Free and Open Source Software News Google! Live! Facebook! StumbleUpon! TwitThis Joomla Free PHP
 

Add comment

Tumia jukwaa ili kutoa maoni ambayo yatasaidia kulijenga taifa letu. Kumbuka, maoni yako yatapitiwa kwanza kabla hayajarushwa hewani!!!!!!


Banner