|
Na Charles Kayoka MWALIMU Julius Nyerere alichukia sana na kutoa hotuba kali dhidi ya wale waliosema afadhali ya mkoloni kuliko serikali hii ya uhuru.
Sina uhakika angesema nini leo, miaka zaidi ya hamsini baada ya uhuru nchi za Afrika bado haziwezi hata kutengeneza sindano ya kufumia kitambaa, achilia kuwa ni chaka la kila aina ya ufisadi na dalili za kutojikwamua. Mimi sisemi afadhali ya mkoloni, bali nasema Afrika haitajikwamua! Kwanza kuna tatizo la uongozi ambao kwa sasa umefunga ndoa na makampuni na serikali za nje. Wamekuwa wawekezaji ndani ya nchi zao kwa kujificha nyuma ya migongo ya wawekezaje, wana hisa huma, wamepata asilimia kumi, na wanashirikiana na wawekezaji kuwaibia wananchi wenzao. Kwa sababu hiyo sio rahisi wa kutumika kama nyenzo za kudhibiti wizi wa rasilimali za nchi. Kama tulivyoona Zaire na kwingineko, nchi za wakubwa zikawatumia viongozi wa nchi zetu kuwafanya watu kuwa masikini zaidi.
Linalokaribiana na uongozi ni kukosa kusema ukweli katika siasa na kwa sababu ya sekta ya siasa na serikali kuwa ndiyo sekta pekee yenye kipato cha uhakika na kukufanya uwe tajiri kwa haraka, wanaojiajiri huko ni wenyewe, na kwa lengo moja tu kutumia uongozi kwa malengo binafsi.
Matokeo yake ni kuona walio madarakani ni ndugu wa damu, wa ushemeji, wa familia, au wa urafiki tu. Na hapo hatuwezi kusemana wala kuambiana kuwa tumekosea. Hatutaendelea! Lakini unawezaje kujenga nchi ambayo haina mikakati kabisa ya kujikwamua ila ina mikakati tu ya kujikimu! Taifa linachofanya ni kusema bora twenda, na kesho ifike, lakini sio tutakuwa wapi miaka hamsini ijayo.
Namna gani tutakuza uchumi kwa kuweka mikakati minene ya uchumi. Naingalia Tanzania ambayo imezungukwa na nchi sita ambazo hazina bahari kabisa, na moja wapo haina miundo mbinu ya kibiashara na serikali yake kuu, lakini hatutumii hiyo kama fursa ya kujenga miundo mbinu ya kuvutia biashara na kuingiza fedha kwa wananchi na hivyo kodi zaidi kwa serikali.
Tatizo ni kuwa wafikiria maendeleo wetu huwa wanaishi jana na leo, na kutaka kuweka kidogo kwa ajili ya kuamkia kesho, hakuna wa kufikiria namna ya kufika mwakani. Hiyo ni kudra ya Mungu, hatupaswi kufikiria. Nchi za magharibi kina siku zinafikiria namna ya kupata maraisi na viongozi vibaraka hapa Afrika, na huwatumia hao kupata maslahi yao na kuyatetea.
Sasa imekuwa ni jambo la sifa kwa viongozi kujipendekeza kwa nchi za magharibi ili kupata kidogi kile kidondakacho kutoka meza ya bwana, lakini huyu bwana humega pande kubwa la rasilimali zatu na kuzihamishia kwake. Afrika inapata nini katika uhusiano huo usio na usawa, zawadi kidogo za magari, fedha za UKIMWI, kujengewa shule, kupea dawa za misaada, na nafasi za masomo ambazo mwanafunzi mmoja hatumii zaidi ya milioni kumi na tano kwa mwaka, na ikiwezekana
wanamchukua pia akafanyekazi kwao. Afrika itawezaje kujikwamua.
|