
| Tahadhari ya wadau wa elimu kuhusu mtihani wa kidato cha pili | Send to a friend |
| Tuesday, 24 January 2012 12:07 |
|
Mulugo akitangaza uamuzi huo wa serikali anasema kuwa “Kuanzia mwaka 2012 mwanafunzi atakayepata wastani wa chini ya asilimia 30 katika Mtihani wa Kidato cha Pili hataruhusiwa kuendelea na Kidato cha Tatu. Atatakiwa kukariri Kidato cha Pili na fursa hii itatolewa mara moja tu,” Anasema na kufafanua: “Mwanafunzi atakayekariri kidato cha pili na kushindwa kufikia wastani wa asilimia 30 ataondolewa katika mfumo rasmi wa Elimu.” Pamoja na msimamo huo wa serikali, wadau wa elimu wanatoa maoni yao mbalimbali juu ya uamuzi huo wa serikali, wengi wao wakiupongeza lakini wakitoa baadhi ya kasoro zinazotakiwa kufanyiwa kazi. Dk Marcelina Chijoriga Mkuu wa Shule ya Biashara,Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Hata hivyo, tatizo lililopo katika mfumo wa elimu Tanzania ni mkanganyiko wa uamuzi. Yale masomo yalikuwa yanamwandaa mwanafunzi kwa masomo ya chuo kikuu, sasa mtu anakuja akiwa hana maandalizi ya awali, hili ni tatizo. Mgongano wa maamuzi kama hayo, ndiyo pia uliofanya kufutwa kwa mtihani wa kidato cha pili na matokeo yake wanafunzi wakawa wanaona hakuna sababu ya kusoma. Wale watoto bado ni wadogo, siyo vizuri kufukuzwa shule lakini wakiwa wanarudia darasa, itawasaidia kujitahidi na kuhakikisha wanafanya vizuri. Kurudisha mtihani huo na kuwataka wanaoshindwa warudie darasa, ni moja ya mambo yatakayowafanya wanafunzi wasome hata kama hawapendi. Kwa kawaida watoto wadogo hawasomi kwa malengo kama watu ambao wapo vyuoni, kwa hiyo ili kuhakikisha hawa watoto wanasoma lazima kuwe na sababu ya kuwafanya wapende ama walazimike kusoma. Lakini kwenye hili jambo la kusema wanaofeli wanapata nafasi moja ya kurudia na wakishindwa wanaondolewa katika mfumo rasmi wa elimu, nadhani haijakaa sawa. Kufanya hiyo ni sawa na kuwatupa hawa vijana, tunaweza kusema kuwa serikali inawakaanga kabisa. Mtoto anaweza kushindwa mfumo wa sekondari, lakini akaweza kwenye vyuo vya ufundi, kwa hiyo badala ya kusema kuwa wataondolewa katika mfumo rasmi wa elimu, ni vyema tukaangalia njia nyingine ya kuwasaidia. Kwa mtazamo wangu, ingekuwa vizuri wale wanaoshindwa, wapelekwe katika vyuo vya ufundi na siyo kuwaondoa kwenye mfumo rasmi wa elimu. Lengo ni kumfanya huyu mtoto awe na stadi za maisha, aweze kujitegemea asiwe ni mzigo kwa wazazi wala serikali. Aloyce Eliakim (Mwalimu Shule ya Sekondari Rafiki iliyopo Tabata,Dar es Salaam) Huu mtihani unafanya wanafunzi wasome kwa bidii, lengo na maisha. Wataona aibu kuachwa na wenzao kidato cha pili, hivyo watajitahidi kusoma ili wasirudie darasa. Lakini suala la kusema watapata nafasi moja ya kurudia mtihani wala watakaofeli kisha waondolewe kwenye mfumo rasmi wa elimu, sikubaliani nao. Kwa mtazamo wangu, ni vyema wakapewa angalau nafasi mbili za kurudia wakishindwa sasa ndiyo serikali iangalie jinsi nyingine ya kuwasaidia ili baadaye wasije kuwa mzigo. Kwa huu msimamo wa kuwapa nafasi moja tu, nadhani itaongeza idadi ya vijana wa mtaani, hilo litakuwa ni tatizo na siyo suluhisho. Wanafunzi wanafeli mtihani kwa sababu nyingi, siyo kuwa wote wanaoshindwa mtihani hawana akili, ni vyema serikali ikajihakikishia kwanza kuwa, mwanafunzi anayeondolewa kwenye mfumo wa shule ya sekondari kweli hawezi. Huu mtihani sasa utafanya wanafunzi wengi wasome kwa bidii. Pia mimi nadhani kusema wanaoshindwa mtihani waondolewe kwenye mfumo rasmi wa elimu ni sahihi pia. Kufeli na kurudia darasa na wanafunzi ambao walikuwa nyuma yako ni aibu, huu mtihani utakuwa ni changamoto kwa wanafunzi kusoma ili wafaulu. Mchujo wa mtihani huu pia utaepusha kuwapo kwa wanafunzi wanaofika hadi kidato cha nne wakiwa hawajui kusoma na kuandika. Usishangae baadaye kunakuwa na watu wamefaulu, wapo kazini lakini hawajui kusoma wala kuandika. Mtihani wa kidato cha pili una maana kubwa kwenye mfumo wa elimu. |



Na Fredy Azzah










