MwanzoContactsEmail
Home Makala Maarifa Prof Omari: Tuige mfumo wa kikoloni kunusuru sekta ya elimu
BOOKMARK THIS PAGE
Prof Omari: Tuige mfumo wa kikoloni kunusuru sekta ya elimu  Send to a friend
Tuesday, 24 January 2012 12:20

MAADHIMISHO ya miaka 50 ya uhuru yamedhihirisha mafanikio ya kujivunia katika sekta mbalimbali ikiwamo elimu.Kwa mfano, katika sekta ya elimu ilielezwa kuwa nchi imepiga hatua kubwa katika ujenzi wa shule, vyuo na uandikishaji mkubwa wa wanafunzi katika madaraja mbalimbali ya elimu, jambo ambalo ni kinyume na ilivyokuwa enzi za ukoloni.

Hata hivyo, mhadhiri mwandamizi mstaafu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Issa Omari,  pamoja na kusifu mafanikio hayo anasema mfumo wa sasa wa elimu haulingani kiubora na ule wa kikoloni.

Akizungumza na mwandishi wetu Gedius Rwiza, Profesa Omari ambaye pia ni msomi bobezi wa fani ya elimu, anaeleza tofauti iliyopo kati ya elimu ya sasa na ile ya kikoloni.

Swali: Unadhani ni mafanikio gani  tumeyapata katika sekta ya elimu kutoka  uhuru mpaka sasa?
Jibu:   Jambo ambalo Serikali imelifanikisha katika sekta ya elimu ni kujenga majengo mengi ambayo hata hivyo kiutaalamu siyo kuboresha elimu.

Kauli kuhusu mafanikio ya ujenzi wa shule, imekuwa  ikitolewa sana na viongozi, lakini maendeleo ya kitaaluma yanazidi kuporomoka siku hadi siku.

Swali: Kwa mtazamo wako, kitu gani kinachangia kuzorota kwa sekta ya elimu nchini?
Jibu: Tatizo kubwa linaloitafuna  sekta ya elimu ni uteuzi wa viongozi na wasimamizi wa elimu wenye uwezo mdogo kuhusu  masuala ya elimu.Ni vigumu kwa mtu ambaye siyo mtaalamu wa masuala ya elimu  kusimamia sekta ya elimu.

Kwa sasa mawaziri wanaochaguliwa siyo wataalamu wa elimu, badala yake wanapoingia madarakani kuiongoza sekta ya elimu, wanahesabu miaka iishe waondoke na siyo kuisimamia sekta ya elimu.

Viongozi wote wanaoteuliwa hakuna mwenye utashi wa kuwakemea watu wanaokwenda kinyume na mahitaji muhimu katika sekta ya elimu.
 
Zamani viongozi waliochaguliwa katika sekta ya elimu, walitakiwa kuwa na historia fulani katika mchango wa  maendeleo ya taifa.

Ukifanya utafiti utakuta idadi kubwa ya viongozi waliopo  katika Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi,  siyo wataalamu wa elimu jambo  linalochangia kutopatikana kwa   elimu bora.

Kutokana na hali  ya elimu kuendelea kuwa mbaya siku hadi siku, kuna kila sababu viongozi wote wanaoteuliwa kushika madaraka katika Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, kuanzia Waziri,Makatibu Wakuu,Wakurugenzi pamoja na wafanyakazi wa ngazi za chini,wawe wamesomea taaluma ya elimu.

Swali: Kuna tofauti gani kati ya elimu ya kikoloni na elimu ya sasa?
Jibu: Kuna tofauti kubwa kati ya elimu ya kikoloni  na elimu  ya sasa. Enzi za ukoloni elimu haikuchakachuliwa hata kidogo na walimu waliokwenda kusomea ualimu ni wale waliofaulu daraja la kwanza na wengine waliteuliwa na wakuu wa shule baada ya kuonekana wana uwezo mkubwa. Hivi sasa  tunasubiri waliopata daraja la mwisho ndio waende ualimu.

Enzi zetu mwalimu wa somo alitakiwa alielewe vizuri,awe amelifaulu vizuri na utaratibu huo ulianzia darasani ambako  wakuu wa shule na walimu wa taaluma walikuwa wanawaandaa wanafunzi ambao wangeweza kuwa walimu.

Aidha, kila   mwanafunzi aliyesikia anakwenda kuwa mwalimu, alijivunia hatua hiyo lakini sasa hivi mwanafunzi anayechaguliwa kwenda kuwa  mwalimu, anajua anakwenda kuteseka.

Hapo ndipo unapoweza kuona tofauti ya elimu ya kikoloni na sasa, maana mtu anayekwenda kuwa mwalimu akiwa kafeli na bado chuoni  anapata alama za chini, unategemea mwanafunzi apate nini akifundishwa na mwalimu huyo?

Asilimia kubwa ya walimu waliopo sasa  hawawezi kupanua akili ya watu kuweza kusonga mbele na kuwa na ubunifu. Mtu  mwenye uwezo mdogo, ni vigumu kumfanya mwanafunzi awe na uwezo mkubwa wa kufikiri, huku ni  kuzidi kupotosha thamani ya mwalimu

Lakini pia zamani sikuona mwanafunzi akikaa chini bila madawati, vifaa vya kufundishia na kujifunzia.Maabara zilitosha na  sikuona mwanafunzi aliyemaliza kidato cha sita akiwa mwalimu  bila kupata mafunzo rasmi ya ualimu. Hivi sasa  mwanafunzi aliyemaliza kidato cha sita, utamkuta anafundisha sekondari hasa hizi za kata, jambo ambalo ni upotoshaji.

Swali: Kwa mujibu wa maelezo yako,ualimu siyo fani ya kujivunia au?
Jibu: Kwanza najivunia kuwa mwalimu na maisha ninayoishi  sasa ni matunda ya kuwa mwalimu. Hata Rais wa kwanza wa nchi hii alikuwa mwalimu.

Alijivunia kuwa mwalimu na sio kwamba alikuwa mwalimu kutokana na kupata alama za chini, bali alikuwa mwenye uwezo mzuri na aliyefaulu vizuri,  lakini kwa sasa hata thamani ya Mwalimu Nyerere imepotea.
Swali: Kuna uwezekano wa kuirudisha elimu ya kikoloni ?

Jibu:  Inawezekana endapo viongozi watakuwa na utashi na kukubali kubadilisha mtazamo  kwamba kazi ya ualimu ni ya watu waliopata daraja la mwisho.

Tunataka  wanafunzi wanaokwenda ualimu wawe ni wale waliopata daraja la kwanza kama ilivyokuwa enzi zile ambapo mtu kuwa mwalimu alitakiwa kuwa amefaulu daraja la kwanza.

Wasifu wa  Profesa Omari
Ni mwenyeji wa mkoa wa Kilimanjaro aliyezaliwa mwaka 1942 na kusoma  kidato cha kwanza hadi cha nne  nne katika shule ya Kati ya Tanga kutoka  mwaka 1959 hadi  1962.

Mwaka 1963 alijiunga na kidato cha sita katika  Shule ya Sekondari Minaki, kabla ya  kudahiliwa na   Chuo Kikuu cha Dar es salaam alikosomea  fani ya ualimu na baadaye kuajiriwa kama mhadhiri.


Add this page to your favorite Social Bookmarking websites
Reddit! Del.icio.us! Mixx! Free and Open Source Software News Google! Live! Facebook! StumbleUpon! TwitThis Joomla Free PHP
 

Comments 

 
0 #3 2012-01-27 08:00
Ni kweli kabisa Prof. yaani kwa sasa ualimu umechukuliwa kama ni kwa mtu aliyefeli. Kwani kuna siku kijana mmoja baada ya matokeo ya kidato cha nne kutoka alipokwaeleza wenzake kijiweni kuwa amefeli wakasema "Yaani umekosa hata ualimu?" Hii inamaanisha kuwa ualimu ni kwa waliofeli/wenye alama za chini.
Totafakari!
Quote
 
 
-1 #2 2012-01-24 16:59
Aaa alaa leo mumeikumbuka UKOLONI....!!!
Quote
 
 
+2 #1 2012-01-24 15:07
Amen Amen Amen Prof. well said.....huu ndio ukweli unaoendelea nchini Tanzania ambapo viongozi wanapeana madaraka kwa ushikaji na sio kutokana na utaaluma walionao na hii imeshusha kwa kiwango kikubwa system ya elimu na afya kwa kiwango ambacho kitahitaji si chini ya miaka 20 na ziada kuirekebisha angalau irudi kwenye baseline... Amenukumbusha babu yangu mdogo anavyojivunia kila apitapo anatambuliwa kama mwalimu aliyetoa matunda ya watu waliofaulu maishani. haya yanaweza kubadilika tu pale viongozi wanaochaguliwa na raisi kutakiwa kupitishwa na bunge baada ya kujadiliwa kama wanafaa au kuwa na uwezo wa kufanya mabadiliko...i hope raisi atakuwa amesoma hii aticle kwani anatia aibu na incapable cabinet aliyonayo....
Quote
 

Add comment

Tumia jukwaa ili kutoa maoni ambayo yatasaidia kulijenga taifa letu. Kumbuka, maoni yako yatapitiwa kwanza kabla hayajarushwa hewani!!!!!!


Banner
Banner