MwanzoContactsEmail
Home Makala Mchakato wa Katiba Mpya Tanzania: Nchi ya mstari wa mbele kwa ukombozi wa bara la Afrika
BOOKMARK THIS PAGE
Tanzania: Nchi ya mstari wa mbele kwa ukombozi wa bara la Afrika  Send to a friend
Friday, 09 December 2011 12:10

 

 

Na Matern Kayera
BAADA ya kuundwa kwa Kamati ya Ukombozi ya OAU mwaka 1963, harakati za kuzikomboa nchi ambazo zilikuwa bado chini ya utawala wa kikoloni zilianza mara moja Barani Afrika. Brigedia Jenerali Mstaafu Hashim Mbita ndiye aliyekuwa Katibu Mtendaji wa Kamati ile ya Ukombozi.

Katika ardhi ya Tanzania, Serikali iliamua kulitumia eneo la Kongwa Mkoani Dodoma kama kituo cha mafunzo ya kijeshi kwa wapigania uhuru wa kutoka vyama vya FRELIMO (Msumbiji), SWAPO (Namibia), MPLA (Angola), PAC na ANC (Afrika ya Kusini), pamoja na ZANU PF kutoka Zimbabwe.
Tofauti ya kufika kwao ilikuwa ni miezi, lakini wapigania uhuru wote walifika Kongwa mwaka 1964.

Wazee, Tito Fungo (90) na Ozmanda  Boma (74) ambao ni wenyeji wa Kongwa, wanasema kabla ya kuja kwa wapigania uhuru katika mji wao, Mwalimu Julius Nyerere alifika kwanza na kuwaomba wawapokee wageni hao ambao nchi zao zilikuwa bado zinatawaliwa na wakoloni.

Baada ya Mwalimu Nyerere kuondoka, baadaye mwaka huo huo (1963), aliyewahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ulinzi, Mh Oscar Kambona alifika Kongwa na kuendelea kuwasisitiza wananchi juu ya umuhimu wa kuwapokea wageni hao kutoka nchi za kusini mwa Afrika.

Kambona aliwaambia wenyeji wa Kongwa katika mkutano wa hadhara aliofanya katika Jengo la TANU kuwa, waafrika wenzetu wa nchi za Msumbiji, Namibia, Angola, Afrika ya Kusini na Zimbabwe bado wanateswa na wanahitaji kupata uhuru, na uhuru wao wataupata kwa mtutu wa bunduki;
Hivyo watakuja Tanzania (Kongwa) kujifunza mbinu za kuwang’oa wadhalimu waliokuwa wanatawala nchi zao, tunaomba wapewe msaada, ushirikiano wa hali na mali.

Kufuatia maombi ya viongozi wa Kitaifa, wazee hao wamesema kwa kuwa asili ya watu wa Kongwa ni ukarimu, maombi yao  yalikubaliwa na hivyo wageni wakafika na kuanza mafunzo  ya kijeshi kwa muda wote waliokuwepo pale.
Kabla ya kuja kwa wapigania uhuru mwaka 1964, Shirika la Kiingereza lililojulikana kama  ‘Overseas Food Corporation’ (OFC) lilifika Kongwa mwaka 1947 na kuanzisha utafiti wa kilimo cha karanga kwa lengo la kufufua uchumi wa Uingereza ambao uliathiriwa na Vita Kuu ya Pili ya dunia.

Mradi huo pia ulikuwa umelenga kuwapatia ajira wanajeshi wa Uingereza waliorudi kutoka vitani. Baada ya utafiti kukamilika, kilimo cha karanga kilianzishwa rasmi mwaka 1948 na kuipa Kongwa umaarufu mkubwa.

Kwa kuwa mashamba yalikuwa yakimilikiwa na wazungu, waafrika walitumika kama vibarua tu katika mashamba yale. Watu wa kutoka Mauritius walikuwa wakifanya kazi za udereva na ufundi; watu wengine waliokuwa wakifanya kazi katika shirika hilo ni Wahindi na Wasomali.
Ili kufanikisha malengo yao, Waingereza  waliamua kujenga reli ya Msagali-Kongwa-Songambele mwaka huo huo 1947. Pia stesheni ya Kongwa nayo ilijengwa.

Kutokana na ukosefu wa mvua kwa miaka mitatu mfululizo, Shirika la OFC liliamua kufunga mradi huo wa kilimo cha karanga. Katika eneo hilo la Stesheni ya Kongwa ndipo walipokuwa wakikaa wapigania uhuru waliotoka Kusini mwa Afrika.
Mahusiano kati ya wapigania uhuru na wenyeji
Wazee, Ozmanda Boma na  Tito Fungo kwa nyakati tofauti wameeleza jinsi mahusiano yalivyokuwa kati yao na wapigania uhuru kwa muda wote waliokaa Kongwa.

Mzee Boma anaweka wazi kuwa wakati huo yeye ndiye alikuwa mpiga picha wao na aliyekuwa akizisafisha pia.  Anaongeza kuwa Samora Machel alikuwa mchangamfu sana na alielewana na watu wengi hata kufikia kujifunza na kuzungumza kigogo.

Kwa upande wake Mzee Fungo anasema wageni wao walikuwa watulivu na hawakuwa na vurugu zozote; walishirikiana nao vizuri.  Amesema kwa mfano ukumbi wa polisi  Kongwa ulijengwa na Wapigania uhuru wa Afrika ya Kusini.
Kwa mujibu wa wazee hao, wapigania uhuru pia walishiriki katika sherehe mbalimbali za kitaifa kama vile Uhuru na Jamhuri, Muungano, Mei Mosi na Sabasaba.

Kushiriki kwao ilikuwa katika kucheza michezo mbalimbali kwa kushirikiana na wananchi; baadhi ya michezo hiyo ilikuwa mpira wa pete na mpira wa miguu. Lakini pia walishiriki katika ujenzi wa Jumba la Maendeleo Kongwa mwaka 1967.
Wapigania uhuru walipohitaji kujifunza lugha ya Kiswahili waliweza kusaidiwa na wenyeji wao. Kwa mfano, Mwalimu Hilda Malogo ametajwa kuwa ndiye alijitoa kikamilifu katika kuwafundisha Kiswahili.

Baadhi ya wanafunzi waliohudhuria katika somo la Kiswahili ni Sam Nujoma, David Ushona, Limo, na Samora Machel; kwa mujibu wa wenyeji wa Kongwa, wanafunzi hawa pia walijifunza lugha ya Kigogo.

Kuwepo kwa wapigania uhuru katika mji wa Kongwa, kulitoa fursa kwa wenyeji kuanzisha shughuli mbalimbali za kibiashara. Biashara kubwa iliyofanyika ilikuwa ni ya vyakula. Wananchi walipata nafasi ya kuwauzia vyakula wapigania uhuru na hivyo kuwa na chanzo cha uhakika cha mapato kutokana na uhusiano mzuri uliokuwepo miongoni mwao.

Aidha, hali ya mahusiano ilienda mbali zaidi hata kufikia hatua ya kuoana kati ya mabinti wa Kongwa na wapigania uhuru. Kwa mujibu wa Mzee Fungo baadhi ya wapigania uhuru wa kutoka Namibia waliondoka na familia zao, yaani wake zao pamoja na watoto.
Kuhusu kushiriki katika mambo ya ibada, Mzee Boma anasema Samora Machel aliwahi kumwambia kuwa hawawezi kujiingiza kwenye mambo ya dini kwani lengo la kuwepo kwao pale lilikuwa ni kupata mafunzo ya kijeshi kwa ajili ya kuzikomboa nchi zao, na kwa kuwa dini zinazuia kuua isingekuwa rahisi kwao kushiriki  katika mambo hayo.

Usimamizi kwa wapigania uhuru
Kwa kuwa Tanzania ilikuwa ndiyo kituo cha kuwahifadhi wapigania uhuru, Umoja wa Nchi za Afrika (OAU) uliamua kumteua ndugu B.M. Kibasa kuwa msimamizi wa shughuli zote za wapigania uhuru akishirikiana na watanzania wengine kama vile Meja Yusuph Mohamed Chongambele, Col. Isack Mwisongo, Lt Maganga na wengine kutoka nchi mbalimbali duniani.

Mafunzo ya kijeshi
Mzee Boma anaeleza kuwa safu ya milima ya Mlanga iliyopo karibu kabisa na eneo la nyumba yake ndiyo iliyokuwa ikitumiwa kwa mafunzo ya kijeshi na wapigania uhuru.

Anasema wapigania uhuru walikuwa wakipita kwenda kwenye mazoezi saa tatu asubuhi na kurudi saa kumi na mbili jioni. Anaongeza kuwa mafunzo hayo yalisimamiwa vyema na wanajeshi wa Tanzania kwani Mkuu wa Kambi alikuwa Meja Chongambele akisaidiana na askari wengine kama vile Kanali Mwisongo.
Aidha amesema wao kama wenyeji wa Kongwa walizoea milio ya risasi na  mizinga, ila walikuwa na wasi wasi sana wa kuangushiwa mabomu na maadui wa wapigania uhuru.

Amesema walikuwa na hatari kwani Wareno walishawahi kukamatwa Kongwa kwa kupotea njia kwani walipoulizwa walisema wametoka Singida na kuelekea Dodoma, lakini walikuwa hawajui Dodoma ni sehemu gani.
Ameongeza kuwa kuwepo kwa wapigania uhuru Kongwa wamejifunza kuwa mapinduzi sio kitu kizuri kutokana na pilika pilika za kijeshi zilizokuwa zikiendelea kwenye mji wao.

Ujenzi wa handaki
Handaki la kihistoria lilijengwa na wapigania uhuru mwaka 1968. Handaki hilo lilikuwa likitumiwa na Samora Machel kama ofisi yake. Kwa maelezo ya Mkuu wa Sekondari ya Kongwa, Bw. Joseph Ilomo, ambako ndipo palikuwa kambi za wapigania uhuru, handaki hilo lilikuwa na njia ya chini kwa chini hadi kwenye nyumba alimokuwa akiishi Samora Machel.

Ameongeza kuwa pembeni kidogo mwa nyumba hiyo kuliwekwa rada ambayo ilikuwa ikimulika pande zote ili kubaini kama kuna adui yeyote aliyekuwa akiwanyemelea. Handaki ambalo Samora Machel alikuwa akilitumia bado lipo mpaka sasa, ingawa uchakavu unashika kasi.
Mbali na handaki hilo, pia madarasa na mabweni yaliyokuwa yakitumiwa na wapigania uhuru  bado yapo ingawa nayo yameanza kuchakaa sana kutokana na utunzaji kuwa duni.

Pia katika eneo la Morisheni kuna makaburi ya wapigania uhuru waliofariki kutokana na maradhi mbalimbali. Wageni wengi hupenda kutembelea maeneo hayo kwa ajili ya kupata historia.

 

 

 

 


Add this page to your favorite Social Bookmarking websites
Reddit! Del.icio.us! Mixx! Free and Open Source Software News Google! Live! Facebook! StumbleUpon! TwitThis Joomla Free PHP
 

Add comment

Tumia jukwaa ili kutoa maoni ambayo yatasaidia kulijenga taifa letu. Kumbuka, maoni yako yatapitiwa kwanza kabla hayajarushwa hewani!!!!!!


Banner
Banner