
| Songe atetea ubingwa wa Bantam | Send to a friend |
| Thursday, 22 December 2011 19:33 |
|
BINGWA wa ndondi za kulipwa uzani wa Bantam wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara, Ramadhani Songe ametetea ubingwa wake kwa kumchakaza Swaleh Masoud kwa TKO katika raundi ya tatu. Katika pambano hilo la raundi 10 lililofanyika juzi kwenye ukumbi wa Ngabomoa katika mji mdogo wa Mirerani, Songe alishinda pambano hilo baada ya Masoud kushindwa kuendelea na mchezo huo ilipokwisha raundi ya tatu. Mamia ya washabiki waliohudhuria pambano hilo la kulipwa lililodhaminiwa na Haki Ellygram walishuhudia Songe akirusha kiufundi masumbwi tangu raundi ya kwanza hadi ya tatu ilipomalizika na Masoud kushindwa kuingia kuendelea na raundi ya nne. Akitumia zaidi na mkono wa kushoto kwa kumpiga ngumi za kidevuni na kichwani, Songe alitawala mchezo huo na kudhihirisha kuwa hana mpinzani hivi sasa kwenye uzito wake wilayani humo, hivyo kutetea ubingwa wake. Katibu wa chama cha ngumi za kulipwa wilayani Simanjiro,Haruna Katuga aliwaomba wadhamini zaidi wajitokeze kudhamini michezo hasa hasa mchezo wa ngumi na wasibobee kwenye udhamini wa mchezo wa soka pekee. Mapambano mawili ya utangulizi yalichezwa kabla ya pambano hilo la Songe na Masoud, ambapo Tall Mbeba Saruji alimgalagaza Oziozi kwa kumpiga kwa pointi 13-7 na Poli alimtwanga Mwachala Mtanga kwa pointi 12-9. Akizungumza baada ya pambano kuu kumalizika, Katibu wa ngumi wilayani humo, Katuga alisema watatafuta mapambano zaidi ya masumbwi ili kunyanyua vipaji na kuuendeleza mchezo huo kwenye wilaya hiyo. Mabondia maarufu nchini wakiwemo Rashid Matumla, Haji Matumla, Stanley Mabesi, Joseph Marwa, David Limbakisye, Andrew George na wengineo wengi wamewahi kucheza mapambano mengi kwenye mji mdogo wa Mirerani wilayani humo. |














