
| Magereza yaisambaratisha Ngome | Send to a friend |
| Thursday, 12 January 2012 17:54 |
|
TIMU ya Magereza imeanza kwa kushindo Kombe la Phoenix Assurance Mapinduzi kwa kuisambaratisha Ngome kwa magoli 8-0 katika mchezo uliofanyika kwenye uwanja wa Lugalo jijini Dar es Salaam. Magereza ilianza mchezo huo kwa kasi na kufanikiwa kufunga goli dakika ya 11 kupitia Castro Mayuma akiunganisha krosi ya Samweli Ebo kutoka upande wa kushoto. Juma Salumu aliipatia Magereza goli la pili dakika ya 20 baada ya mabeki wa timu ya Ngome kuchelewa kuokoa mpira katika eneo lao hatari, hadi mapunziko Magereza walikuwa mbele kwa magoli 2-0. Kipindi cha pili kilipoanza Magereza waliendelea kuisakama Ngome na kufanikiwa kupata bao la tatu kupitia kwa Mayuma akiunganisha pasi ya Samweli Ebo. Naye Ebo alifunga goli la nne akimalizia pasi na Federick Okoth, karamu hiyo ya Magereza ilimaliziwa kwa bao la Mayuma na Ebo alifunga kwa njia ya penati baada ya beki wa Ngome, Hussein Mdee kuokoa mpira kwa mguu. Katika mchezo mwingine uliochezwa jana timu ya Magereza B iliichapa Dsm Institute magoli 6-3, magoli hayo kwa timu ya Magereza yalifungwa na Titusi Murwa dakika 10 na 60, Henry Mlay dakika 18 na 64 na Njogu Joshua (70). Mengine yalifungwa na Saidi Nguvumali (28) , Mufadal Bhaee (30) wakati magoli ya Dsm Institute yalifungwa na Nabeela Mawji mawili (41 na 46) na Jacinto D' Melloona alifunga moja. Michuano hiyo itaendelea leo kati ya TPDF na Magereza, Zanzibar na Magereza B huku Dsm Institute dhidi ya Dar Khalsa na mchezo wa mwisho utakuwa kati ya Moshi Khalsa dhidi ya Ngome. |














