Mimi Mars ataja sababu za kutoonekana tena kwenye Jua Kali

Muktasari:

  • Licha ya kutokuwepo kwenye tamthilia hiyo ameahidi mashabiki kuwa ataonekana kwenye sirizi inayofuata. Kwa sasa nafasi yake imechukuliwa na mwigizaji Elizabeth Michael maarufu kama Lulu.

Kutokana na malalamiko ya mashabiki wa mwigizaji na mwanamuziki Marianne Mdee 'Mimi Mars',  juu ya kutoonekana tena kwenye tamthilia ya Jua Kali, hatimaye msanii huyo ameweka wazi kwa kueleza sababu iliyofanya asiwepo kwenye tamthilia hiyo na nafasi yake kupewa mtu mwingine.

Akizungumza katika video fupi aliyoichapisha kwenye ukurasa wake rasmi wa Instagram amesema kuwa kutokana na ajali aliyopata daktari amemshauri kupumzika kwanza na kuachana na kazi ngumu zinazochukua muda mwingi ambapo ametaja uigizaji ni moja wapo.

"Kwanza kabisa hamtaweza tena kuniona kwenye Jua Kali kama Maria lakini nimefurahi sana kuweza kuwa mmoja wa timu ile na Lamata Village, kwa kweli nimeinjoi sana kuigiza kama Maria na kuona upendo wenu na sapoti yenu imeweza kunisaidia hata katika kazi yangu ya uigizaji, lakini tangu nimepata ajali nilipata tatizo la kichwa na akili kwa hiyo bado naendelea kupona kidogo kigogo daktari aliniambia sitakiwi kufanya kazi inayotumia nguvu nyingi na muda mwingi uigizaji hilo ni la kwanza"

Licha ya kutokuwepo kwenye tamthilia hiyo ameahidi mashabiki kuwa ataonekana kwenye sirizi inayofuata. Kwa sasa nafasi yake imechukuliwa na mwigizaji Elizabeth Michael maarufu kama Lulu.

Pamoja na hayo Mimi Mars, amesema kazi ambazo anaweza kufanya kwa sasa ni muziki, ushereheshaji na utangazaji wa bidhaa. Msani huyu ameachia ngoma mpya iitwayo  ‘Till I Die’,  ambayo hadi sasa inazaidi ya watazamaji laki sita kwenye mtandao wa YouTube huku ikiwa na siku kumi na moja tangu kuachiwa kwake.